Baraka FM

Naibu Waziri Maji kushiriki mkutano wa 13 wa ubunifu wa teknolojia za maji

19 February 2024, 09:54

Na mwandishi wetu, London Uingereza

Naibu Waziri wa Maji, Mheshimiwa Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) amewasili Nchini Uingereza, kwa ajili ya kushiriki Mkutano wa 13 wa ubunifu wa Teknolojia za maji kwa Mwaka 2024( World Water-Tech Innovation Summit) akimuwakilisha Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso(Mb)

Aidha, Mkutano unatarajia kujadili uwekezaji endelevu kwenye miradi ya maji, uendelezaji wa Taasisi za Maji, ubunifu wa mifumo ya usimamizi wa miradi ya maji, usimamizi wa majanga yanayotokana na maji, mifumo ya uhimilivu wa maji katika mabadiliko ya tabianchi pamoja na ubunifu katika uendelezaji wa rasilimali za maji.

Mkutano huo utawaunganisha wadau wa Sekta ya Maji Duniani wakiwemo wafadhili na makampuni yanayozalisha Vifaa Vya maji, Teknolojia za maji pamoja na Madawa ya kusafisha na Kutibu Maji.

Pia, Mhe. Mahundi amewasili kwenye Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Uingereza na kupokelewa na Balozi Mhe. Mbelwa Kairuki

Hata hivyo, katika safari hiyo ya Nchini Uingereza, Mhe. Mahundi aeongozana na Mkurugenzi wa Uandaaji wa Miradi, Uratibu na Usimamizi wa Mazingira.