Baraka FM

Fisi aua watatu, ajeruhi, watano wafa maji Mbeya

8 April 2024, 19:15

Jeshi la polisi mkoa wa Mbeya limeendelea kutoa wito kwa wazazi na walezi kuchukua tahadhari kwa watoto kwa kuhakikisha wanaweka uangalizi mzuri kwa watoto wao.

Na Ezra Mwilwa

Watoto watatu wameuwawa na wengine kujeruhiwa na mnyama aina ya fisi katika kitongoji cha Gengeni kilichopo kata ya Kambikatoto, tarafa ya Kipembawe, wilaya ya Chunya mkoa wa Mbeya.

Taarifa ya tukio hilo imetolewa na kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya SACP Abdi Issango kwa vyombo vya habari.

Kamanda Issango amesema tukio hilo limetokea mnamo April 07, 2024 na familia ya iliyoathiriwa ni ya Shigela Ngasa [45].

Amesema baada ya tukio hilo la mauaji kutokea mnyama huyo aliwajeruhi wazazi wa watoto hao ambao ni Shigela Ngasa [baba] na mke wake aitwaye Limi Masanja [33] wote wakazi wa Gengeni. Baada ya tukio hilo fisi huyo aliua kondoo wawili na kisha akakimbia uelekeo wa hifadhi ya Rungwa eneo la Kambikatoto.

Sauti ya kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya SACP Abdi Issango

Wakati huo huo, mnamo April 07, 2024 katika kitongoji cha Katagho kilichopo kijiji cha Ngeleka, kata ya Makwale, tarafa ya Ntebela, wilaya ya Kyela mkoa wa Mbeya, watoto watano wamefariki  dunia wakati wanapatiwa matibabu katika zahanati ya Uhai Baptist baada ya kuzama ndani ya dimbwi la maji lililopo kwenye shamba la kakao lenye ukubwa wa ekari nne.

Aidha amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa watoto hao walienda kuogelea kwenye dimbwi lililojaa maji kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha ndipo walizidiwa na maji na kuzama, walipiga kelele kuomba msaada wa kuokolewa na wananchi lakini tayari walikuwa katika hali mbaya.

Sauti ya kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya SACP Abdi Issango