Baraka FM
Baraka FM
24 June 2025, 05:26

Wanasema ili uweze kufanikiwa kufanya jambo fulani unapaswa kuweka Imani, ndivyo ambavyo waumini wa dini mbalimbali wanapaswa kuwekeza kwenye maombi kuelekea uchaguzi Mkuu October mwaka huu .
Na Hobokela Lwinga
Viongozi wa dini nchini wametakiwa kusema kweli ya Mungu juu ya matukio maovu yanayotendwa na baadhi ya watu wasiolitakia mema taifa la Tanzania.
Rai hiyo imetolewa na Askofu wa kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la kusini magharibi mch.Robert Pangani katika ibada ya maombi ya kuombea kanisa na taifa iliyoandaliwa na idara ya uinjilisti na mission ya jimbo hilo iliyofanyika katika ushirika wa Chunya mjini uliopo wilaya ya Chunya mkoani Mbeya.

Aidha Katibu wa idara ya uinjilisti na mission ambaye pia ni Katibu idara ya uwakili katika kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la kusini magharibi mch paul Mwambalaswa amesema lengo la Maombi hayo ni kuombea kanisa na taifa na yatakwenda kila wilaya ya kanisa hilo kwa kuanzia kwenye shirika.

Baadhi ya washiriki wa ibada hiyo mch.Elisha Mzumbwe wa ushirika wa Tumaini uliopo uyule Mbeya na Joyce Msyani ambaye ni muumini katika kanisa hilo wamesema Kanisa likiwa na nguvu ya kuomba husabisha taifa kuwa na amani.

Ibada hiyo iliyofanyika katika kanisa la Moravian ushirika wa Chunya ni ya pili katika mwendelezo wa ibada za maombi ikitanguliwa na ibada ya kwanza iliyofanyika katika ushirika wa Jakaranda (cathedral )huku ibada nyingine ikitarajiwa kufanyika katika kanisa la Moravian ushirika wa Mlima reli Mbalizi mwezi julai mwaka huu.