Baraka FM
Baraka FM
26 August 2025, 20:06

Kutokana na maendeleo ya sayansi na tekinolojia baadhi ya makundi ya vijana wamekuwa wakitumia maendeleo hayo kwa mlengo chanya na hasi.
Na Hobokela Lwinga
Askofu wa Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la Kusini Magharibi, Robert Pangani, amewataka wanafunzi wahitimu Darasa la Saba kuepuka makundi yasiyo na maadili mara baada ya kumaliza mitihani yao ya kuhitimu elimu ya msingi.
Rai hiyo ameitowa wakati wa sherehe ya mahafali ya nne ya Darasa la Saba katika shule ya msingi sunrise iliyopo mkoani Songwe,ambapo amewakumbusha wanafunzi hao kuendelea kuwa na nidhamu, heshima na maadili mema wanapokuwa nyumbani wakisubiri matokeo yao.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Stephen Mwasongwe, amesema shule hiyo imekuwa ikiwapa wanafunzi elimu jumuishi inayojumuisha stadi za maisha kama vile kilimo na matumizi ya TEHAMA, ili kuwaandaa wanafunzi kuendana na mabadiliko ya kisasa ya sayansi na teknolojia.

Naye Tunosye Mboya akizungumza kwa niaba ya wazazi wa wahitimu, ameushukuru uongozi wa shule kwa juhudi kubwa katika malezi, maadili na elimu bora kwa watoto wao.

Mmoja wa wanafunzi wahitimu wa Darasa la Saba katika shule hiyo Clara Belema ameeleza baadhi ya changamoto wanazokumbana nazo, ikiwemo upungufu wa vifaa vya kujifunzia na miundombinu ya shule, huku akitoa wito kwa wadau kusaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia.
