Baraka FM
Baraka FM
17 June 2025, 05:46

Kufuatia tamko la waziri wa TAMISEMI mh Mohamed Mchengerwa kuagizi ifikapo june 20 kuvunjwa kwa mabaraza ya madiwani Mkuu wa mkoa wa Mbeya akutana na madiwani Halmashauri ya jiji la na kuwapongeza
Na Ezra Mwilwa
Halmashauri ya Jiji la Mbeya imepongezwa kwa kuongeza kiwango cha ukusanyaji wa mapato kutoka bilioni kumi na tano miaka minne iliyopita mpaka kufikia kiasi cha shilingi bilioni ishirini nane ambayo sawa asilimia mia moja na kumi(110%)mwaka huu wa fedha 2024/2025.
Akizungumza wakati wa baraza la madiwani kupitia hoja za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali(CAG),Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe.Dkt Juma Homera amempongeza Mkurugenzi Bw.John Nchimbi,watendaji,Mstahiki Meya Mhe.Dormohamed Issa na Baraza la Madiwani kwa jitihada walizozifanya mpaka kufikia kiwango hicho kwa mwaka huu wa fedha 2024/2025.

Aidha Mkuu wa Mkoa ametoa maelekezo kwa watendaji kuhakikisha wanatumia vyema fedha za serikali wakati madiwani wanaelekea katika mchakoto wa uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika mwezi Oktoba kwa kumchagua Rais,wabunge na Madiwani baada ya kuvunjwa kwa mabaraza ya Halmashauri zote nchini mnamo Juni 20 mwaka huu.
Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya Bi.Anamary Joseph amekiri kupokea maelekezo hayo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa na kuahidi kwenda kuyafanyia kazi ili kuzilinda na kuzisimamia vyema fedha za serikali kwa maslahi ya Umma.

Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya Mhe.Dormohamed Issa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan kwa fedha za miradi ya maendeleo jijini Mbeya na kuwa pongeza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Mhe.Dkt Juma Homera, Mhe.Dkt Tulia Ackson mbunge na Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe.Beno Malisa kwa kulisimamia vyema Jiji la Mbeya katika kutekeleza majukumu yake na kuleta tija kwa jamii.
