

29 January 2025, 09:05
Kukamilika kwa Hospitali ya Wilaya ya momba kutakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa maeneo ya kata za Chitete na Msangano, hivyo kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.
Na Mwadishi wetu ,Songwe.
Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Daniel Chongolo, amepongeza maendeleo ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Momba iliyopo katika Kata ya Chitete, akibainisha kuwa licha ya kasoro ndogo zilizojitokeza, majengo yaliyojengwa ni mazuri na yanaonesha kuwa na ubora.
Ametoa pongezi hizo leo Januari 28, 2025 wakati akizungumza na watumishi wa Hospitali hiyo ambayo tayari imeanza kutoa huduma mara baada ya kumaliza kufanya ukaguzi, ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku moja kwa ajili ya kukagua miradi ya maendeleo katika Halmashauri hiyo.
“Tumekuja hapa kukagua na kujiridhisha kuhusu matumizi ya fedha ambazo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amezishusha huku chini kwa ajili ta miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Momba ili kuboresha
huduma za jamii” Alisema Chongolo.
Kwa mujibu wa taarifa ilizotolewa na Mganga Mfawidhi (MOI) wa Hospitali ya Wilaya hiyo, Dkt. Faraja Mwinuka, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Fabian Manoza,
ujenzi wa ulianza kutekelezwa Aprili 2024, kwa gharama ya shilingi milioni 796, na unatarajiwa kukamilika Januari 2025 baada ya mkandarasi kuomba nyongeza ya muda kufuatia changamoto ya kusafirisha vifaa vya ujenzi.
Dkt. Mwinuka alisema, ujenzi huo unahusisha majengo manne, yakiwemo jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la kufulia, na stoo ya dawa.
Dkt. Mwinuka aliongeza kuwa, hadi sasa, jumla ya shilingi milioni 583 zimetumika katika ujenzi, huku hatua za mwisho zikiendelea, ikiwemo uwekaji wa marumaru na kufunga milango.
Katika hatua nyingine, Chongolo alitumia fursa hiyo kukabidhi gari la wagonjwa lililotolewa na serikali kwa ajili ya kutumika katika Hospitali hiyo na kuhimiza utoaji wa mafunzo kwa madereva wanaotumia magari yanayonunuliwa na serikali kwa gharama kubwa.