Baraka FM

Wananchi 42,000 kunufaika na mradi wa maji Itagano Mwansekwa

26 August 2024, 15:03

Kiongozi wake Ndg: Godfrey Mnzava(kushoto) akisoma jiwe la masingi ibada ya mwenge kuzindua mradi wa chanzo cha maji Itagano Mwansekwa(picha na Hobokela Lwinga)

Kiongozi wa Mwenge amempongeza Ubora wa Mradi huo na kuwaomba Wananchi kutunza vyanzo vya Maji.

Na Hobokela Lwinga

Mwenge wa Uhuru 2024 kupitia kwa Kiongozi wake Ndg: Godfrey Mnzava na timu yake umeweka Jiwe la Msingi Mradi wa Maji Itagano-Mwansekwa unaogharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mfuko wa Taifa wa Maji kwa gharama ya Sh. 5,153,937,498. Halmashauri ya Jiji la Mbeya.

Katika Taarifa iliyosomwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mbeya kwaniaba ya CPA Gilbert Kayange Amesema Utekelezaji wa mradi ulianza mwezi Machi 2023 na unatarajiwa kukamilika mwezi Disemba 2024.

Mradi huu utahudumia wananchi wapatao 42,000 waishio Kata za Mwasenkwa, Iganzo na Ilemi.

Taarifa hiyo imefafanua juu ya kazi zilizopangwa kufanyika na hatua za utekelezaji ambazo ni kama ifuatavyo:-
Ujenzi wa banio za maji mbili katika Mto Hanzya na Hasara. Utekelezaji umekamilika.

Ununuzi na ulazaji wa bomba kuu (Chuma na HDPE inchi 4) na viungio vyake kutoka kwenye vyanzo vya Mto Hanzya na Hasara hadi kwenye chujio la kutibu maji kwa umbali wa Kilomita 3.8. Utekelezaji umekamilika.
Ujenzi wa chujio la kutibu maji (Flocculator na Sedimentation Tank). Utekelezaji umekamilika.

Ununuzi wa bomba za kusambaza maji za Chuma na HDPE zenye kipenyo cha inchi 10, 4, 3, 2.5, 2, 1.5 na 1 zenye urefu wa Kilomita 53.2 pamoja na viungio vyake. Utekelezaji umekamilika.

Ununuzi wa dira za maji 12,000 pamoja na viungio vyake. Utekelezaji umekamilika.
Ujenzi wa tangi la kuhifadhi maji yaliyotibiwa lenye ujazo wa Lita Milioni 1.5. Utekelezaji umefikia asilimia 12.

Kwa ujumla wake utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 82 na umeanza kutoa huduma ya maji na Kaya 348 zimeunganishwa.

Kazi zinazoendelea kwa sasa ni kusogeza huduma kwa wananchi kwa kuchimba na kulaza bomba za kusambaza maji kwa wananchi na ujenzi wa tangi la kuhifadhi maji.

Hadi sasa kiasi cha Sh. 2,522,707,181.95 kimepokelewa kutoka Mfuko wa Maji wa Taifa ambazo zimetumika kugharamia kazi za mradi.

Kiongozi wa Mwenge amempongeza Ubora wa Mradi huo na kuwaomba Wananchi kutunza vyanzo vya Maji.