Baraka FM

Serikali yaombwa kubadili mfumo wa udahili wanafunzi vyuo vya elimu ya juu

3 June 2024, 12:54

Askofu Robert Pangani akisalimiana na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati mara baada ya kubarikiwa kuwa askofu kamili(picha na Hobokela Lwinga)

Kanisa la Moravian Tanzania Jimbo la kusini magharibi limepata askofu mpya baada ya kustaafu kwa aliyekuwa askofu wa Jimbo hilo Dkt.Alinikisa Cheyo.

Na Hobokela Lwinga

Askofu mpya wa Kanisa la Moraviani Tanzania Jimbo la kusini magharibi Robert Pangani ameiomba serikali kuona umuhimu wa kubadili mfumo wa udahili wa wanafunzi katika vyuo vya elimu ya juu nchini, ili kuviwezesha vyuo binafsi kupata wanafunzi sawa .

Askofu Pangani ametoa ombi hilo muda mfupi baada ya kuwekwa wakfu kuwa askofu wa tatu wa Kanisa la Moraviani Tanzania Jimbo la Kusini magharibi amesema chuo kikuu cha Theofilo Kisanji kimekumbwa na mdororo wa wanafunzi kutokana na mfumo wa udahili wa wanafunzi nchiini kutokuwa sawa.

Askofu Pangani amesema mabadiliko ya mfumo wa udahili yameathiri vyuo vingi kwani udahili ungekuwa unafanyika kama unavyofanyika kwa vyuo vikuu kupitia serikali kwa kuvipelekea wanafunzi vyuo hivyo vikuu.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati (katikati)akipanda mti wa kumbukumbu katika chuo Kikuu Teofilo Kisanji TEKU,kulia ni Askofu Robert Pangani kabla ya kuwekwa wakfu(picha na Hobokela Lwinga)

Hata hivyo Askofu Kiongozi wa Kanisa la Moraviani Tanzania mchungaji Conrad nguvumali ameipongeza serikali ya mkoa wa Mbeya chini ya mkuu wa mkoa kwa kukinusuru chuo kikuu cha Theofilo Kisanji-TEKU ambacho kimepitia changamoto za kukosa wanafunzi.

Hata hivyo mgeni rasmi katika hafla hiyo Naibu waziri na waziri wa nishati Dkt.Doto Biteko amewataka watanzania kutokugawanywa kwa itikadi za dini wala vyama vya siasa.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati (picha na Hobokela Lwinga)