Nuru FM
Nuru FM
13 March 2026, 9:00 am

Mtuhumiwa amekamatwa kwa haraka baada ya maagizo yalitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Heri James, aliyesisitiza hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi ya wahusika wa tukio hilo.
Na Hafidh Ally
Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa limemkamata mtuhumiwa wa Ubakaji na mauaji ya kikatili ya mwanafunzi wa darasa la saba aliyekuwa akisoma katika Shule ya Msingi Zizi la Ng’ombe iliyopo Kata ya Isakalilo, Manispaa ya Iringa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa (SACP) Allan Bukumbi amesema mtuhumiwa aliyekamatwa ni Benjamin Kikula ambaye ni baba mdogo wa marehemu na ndiye aliyekuwa akimlea tangu akiwa mdogo ambapo uchunguzi wa awali unaonesha kuwa tukio hilo la kusikitisha limetokea ndani ya familia.
Aidha Kamanda Bukumbi amewataka wazazi na walezi kuongeza umakini katika malezi na uangalizi wa watoto wao ili kuwakinga dhidi ya vitendo vya ukatili na unyanyasaji.
Kwa upande wake Mkuu wa Dawati la Jinsia Mkoa wa Iringa, Elizabeth Swai, amewataka wanawake na watoto kuwa waangalifu hata kwa watu wa karibu ndani ya familia.
Wakati haya yakijiri Jeshi la Polisi limegusia tatizo la baadhi ya waganga wa kienyeji kuwa chanzo cha matukio ya ukatili wa kijinsia huku likiagiza waganga hao kujisajili na kufanya kazi kwa kufuata taratibu na sheria za nchi.