Nuru FM
Nuru FM
3 February 2026, 9:55 am

“Jamii inayopambwa na misingi ya haki itakuwa mfano kwa wengine na kila mtu atataka kuwa sehemu yake”
Na Hafidh Ally
Mahakama Zimetajwa kuwa na nafasi ya kipekee katika kuhakikisha wananchi wananufaika na ustawi wa kweli hasa katika Utoaji wa haki ili kujenga jamii yenye amani, mshikamano na maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi.
Hayo yamezungumwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Iringa Mhe. Dunstan Beda Ndunguru katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini na kuongeza kuwa Mahakama ina dhamana ya kusimamia haki kwa kuzingatia misingi ya utawala wa sheria, jambo litakaloongeza imani ya wananchi kwa taasisi za haki.
Mhe. Ndunguru amesema Mahakama itaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha utoaji wa huduma zake ili kuhakikisha mashauri yanapatiwa maamuzi kwa wakati.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James, amesema Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana na Mahakama kwa kutenga maeneo pamoja na kuboresha miundombinu ya kimahakama, ili kupanua wigo wa huduma hizo na kuzifikisha kwa wananchi wengi zaidi.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Kanda ya Iringa, Wakili Moses Ambindwile amesisitiza umuhimu wa Mahakama kuendelea kutoa maamuzi kwa haki, uwazi na bila upendeleo.
