Nuru FM
Nuru FM
18 December 2025, 12:16 pm

Kilimo cha parachichi kimetajwa kuwa mkombozi kwa kuimarisha kipato cha vijana.
Na Adelphina Kutika
Serikali ya Mkoa wa Iringa imewahimiza vijana kuchangamkia fursa za kilimo cha parachichi kama njia ya kujipatia ajira, kipato na kuboresha maisha yao.
Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua shamba darasa la uzalishaji wa miche ya parachichi linaloendeshwa na kikundi cha Mseke Stars kupitia mradi wa Skills for Employment Tanzania (SET) unaotekelezwa na Swisscontact, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James, amesema kuwa vijana wana uwezo mkubwa wa kufanya kazi kwa bidii wanapopata fursa na mazingira rafiki.
Mhe. Kheri amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuwaunga mkono vijana kwa kuwapatia mafunzo, ujuzi na zana za kazi, akibainisha kuwa kilimo ni sekta muhimu inayotoa fursa nyingi za kiuchumi na ajira.

Nae Mwenyekiti wa kikundi cha Mseke Stars, Bi. Angel Mhema, amesema kitalu chao kina jumla ya miche 3,860 na mradi umeongeza fursa za kujitegemea kiuchumi.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Bi. Saumu Kweka, amesema kuwa Halmashauri itaendelea kushirikiana na vikundi vya vijana pamoja na wadau wa maendeleo ili kuhakikisha miradi hiyo inakuwa endelevu na kuleta matokeo chanya kwa jamii.
Kupitia mradi huo, vijana 30 waliopata mafunzo wanatarajiwa kuwafikia zaidi ya vijana 100, hali itakayosaidia kuimarika kwa uchumi wa vijana na jamii kwa ujumla.