Nuru FM
Nuru FM
27 October 2025, 8:43 am

Mikopo hiyo imetolewa kupitia asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri hiyo katika kipindi cha miezi tisa.
Na Godfrey Mengele
Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo mkoani iringa imetoa mikopo yenye thamani ya Shilingi bilioni 1.7 kwa vikundi 104 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, kama sehemu ya utekelezaji wa agizo la Serikali ya Awamu ya Sita la kuyajengea uwezo wa kiuchumi makundi mbalimbali katika jamii.
Akizungumza wakati wa hafla ya utoaji wa mikopo hiyo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo mkoa wa iringa, Scholastica Gibore, amesema hatua hiyo inalenga kuwawezesha wanufaika kuanzisha na kukuza miradi ya uzalishaji mali, kuongeza kipato na kuboresha maisha yao.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Estomin Kyando, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha fedha zinazotolewa zinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa, huku akisisitiza uwajibikaji na nidhamu ya kifedha kwa vikundi vilivyonufaika.
Baadhi ya wanufaika walioshiriki katika hafla hiyo wameeleza namna mikopo hiyo imebadilisha maisha yao ambapo miongoni mwao ni Juma Kassim, mmoja wa wanachama wa kikundi cha bodaboda, akisema kuwa wameweza kununua pikipiki kadhaa ambazo zimewasaidia kuongeza kipato na ajira kwa vijana.