Nuru FM
Nuru FM
9 October 2025, 5:17 pm

“Mikopo hiyo inaenda kuwanufaisha kiuchumi vijana, wanawake na watu wenye ulemavu”
Na Hafidh Ally
Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imefanikiwa kukabidhi mikopo yenye thamani ya Tsh. Milioni 240 katika robo ya kwanza kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa vikundi 28.
Hayo yamezungumzwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa Bi. Zaina Mlawa ambapo amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utoaji wa Mikopo ya asilimia kumi ya mapato ya ndani ya halmashauri kwa makundi ya Wanawake, Vijana na Watu wenye ulemavu.
Bi.Mlawa amesema jumla ya Tsh. Milioni 240 Zimetolewa katika robo ya kwanza kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa vikundi 28 venye jumla ya wanufaika 121 wa mikopo ili kuwanufaisha kiuchumi.
Naye Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Bi. Mwatumu Dossi amesema mafunzo ya siku 2 waliyotoa yamelenga kuwajengea uwezo wanufaika wa mkopo na amewataka kutumia fedha hizo kwa malengo kusudiwa na kurejesha kwa wakati ili wengine wanufaike na mikopo hiyo.
Wanufaika wa mikopo wamemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwajali na kuwainua kiuchumi kupitia mikopo hiyo huku wakiahidi kutumia elimu waliyoipata katika mafunzo ya kuendesha biashara zao kwa ubunifu ili kurejesha mikopo hiyo kwa wakati.