Nuru FM

TCRA yataka hisabati kutumika katika uchumi wa kidigitali

4 September 2024, 10:59 am

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dr Jabir Bakari akizungumzia kuhusu mfumo wa kidigitali katika ufundishaji. Picha na Adelphina Kutika.

Na Adelphina Kutika

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewataka Walimu wa Hesabu kuwaandaa wanafunzi na vijana kujikita katika masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM) ili kupata fursa ya kushiriki maendeleo ya Dunia katika zama hizi za kidijiti.

Hayo yamebainishwa na mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dr Jabir Bakari  katika Mafunzo ya Muda Mfupi kwa Walimu wa Hisabati Tanzania Yaliyofanyika katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa(MUCE) Mkoani Iringa na kusema kuwa hesabu ni msingi wa sayansi na teknolojia, na katika ulimwengu unaobadilika haraka wa teknolojia, uchumi wa kidijiti unakuwa injini muhimu ya ukuaji wa kiuchumi.

Sauti ya Bakari

Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Waziri Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, Mohamed Mchengerwa, Afisa Elimu Taaluma wa Mkoa wa Iringa, Hansi Mgaya, amewataka wakuu wa shule za kuhakikisha wanakuwa na klabu za Hisabati ili kufanya vizuri katika somo hilo.

Sauti ya Afisa Elimu

Kaimu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Deusdedit Rwehumbiza, amesema walimu wa hisabati wanapaswa kuwa na jukumu la kuhakikisha  wanafunzi  wanapata maarifa hayo muhimu kwa ajili ya mafanikio ya baadaye.

Sauti ya Profesa

Mwenyekiti wa (CHAHITA,) Dk Said Sima, amesema mafunzo hayo yanalenga   walimu wa hisabati wanakuwa na uwezo wa kuingia katika uchumi wa kidijiti na kuwasaidia wanafunzi wao kufanya vyema.

Sauti ya Mwenyekiti CHAHITA

Hata hivyo Chama cha Hisabati Tanzania (CHAHITA), huwakutanisha wataalamu hao kutoka mikoa yote nchini kwa malengo mbalimbali, ikiwa  na kutoa mafunzo kwa walimu wa hisabati ili kuongeza ujuzi na maarifa yao katika kufundisha somo hilo .

MWISHO