Mpanda FM
Mpanda FM
18 June 2026, 12:21 pm

“Amewasihi wafanyabiashara na wazalishaji wa bidhaa kuzingatia miongozo na taratibu zinazotolewa na mamlaka hiyo”
Na Ben Gadau -Katavi
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kanda ya magharibi limeteketeza bidhaa feki na bidhaa zisizokidhi viwango zilizokamatwa katika manispaa ya Mpanda mkoani Katavi.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, afisa mdhibiti ubora kutoka TBS Kanda ya magharibi, Ezekiel Mubito, amewasihi wafanyabiashara na wazalishaji wa bidhaa kuzingatia miongozo na taratibu zinazotolewa na mamlaka hiyo ili kuhakikisha bidhaa zinazowafikia wananchi ni salama na zenye ubora unaokubalika.
Amesema kuendelea kuuza bidhaa zisizokidhi viwango ni hatari kwa afya ya walaji na kunaweza kusababisha madhara makubwa kwa jamii.
Kwa upande wake, afisa afya wa manispaa ya Mpanda ambaye pia ni mratibu wa TBS katika manispaa hiyo, Erick Kisaka, amewataka wananchi kuepuka matumizi ya bidhaa zilizokwisha muda wake wa matumizi, akieleza kuwa zinaweza kusababisha madhara mbalimbali ya kiafya kwa watumiaji.
Zoezi hilo ni sehemu ya operesheni zinazoendelea kufanywa na TBS, ikiwa ni maandalizi ya kuelekea maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa shirika hilo.