Mpanda FM

Katavi waililia serikali kuhusu uvuvi

22 April 2026, 4:07 pm

Baadhi ya wananchi wa kitongoji cha Kabage. Picha na Samwel Mbugi

“Tunakuomba mama Mkuu wa Mkoa hili suala ulifuatilie”

Na Samwel Mbugi

Baadhi ya wananchi wa kitongoji cha Kabage kata ya Sibwesa wilaya ya Tanganyika wameiomba serikali kuwaruhusu kufanya shughuli za uvuvi katika bwawa lililopo Kabage ambalo limekuwa likitumika miaka mingi kuwapatia mboga na kujiingizia kipato.

Wakizungumza na Mpanda radio FM wamesema bwawa hilo limekuwa likitumika kila msimu wa mvua kujipatia kipato lakini msimu huu wamekataliwa na watu wa hifadhi kufanya uvuvi katika eneo hilo lilipo katika mashamba ya kijiji cha Kabage.

Sauti za wananchi

Kwa upande wake mwenyekiti wa kitongoji cha Kabage Paul Maiko Kapaya amesema changamoto hiyo iliibuka tangu mwaka jana baada ya afisa wa uhifadi kufika eneo hilo na kubaini kuwa boko wanaoingia katika mashamba ya wanachi wanapitia katika eneo hilo.

Nae afisa uhifadhi wa wanyama pori Ally Yongolo amesema uvuvi unaofanyika katika bwawa hilo ni uvuvi ambao hauruhusiwi na marufuku hiyo ilipigwa toka mwaka jana na mamlaka husika katoka serikalini

Hata hivyo afisa uvuvi wilaya ya Tanganyika Dismas Kessy amesema wanaruhusiwa kufanya shughuli za uvuvi kwa kufuata utaratibu wa kuwa na vibali pamoja na kutokutumia vyandarua.