Nuru FM
Nuru FM
3 April 2026, 10:26

Wananchi wa Kijiji cha Mangawe Kilichopo Jimbo la Ismani wanatarajia kunufaika na Mradi wa Maji ya Mkopo usiokuwa na riba.
Na Hafidh Ally
Shirika lisilo la Kiserikali la Idydc Mkoani Iringa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira limefika Katika Kijiji cha Mangawe kwa ajili ya kuwapatia mkopo wa kuunganishiwa huduma ya maji safi wananchi wa eneo hilo.
Wakizungumzia Fursa hiyo baadhi ya wananchi wa Kijiji chA Mangawe Kata ya Ngang’oro Wilaya ya Iringa wamesema kuwa wengi wao wanashindwa kumudu gharama za kulipa maji kwa mkupuo hivyo shirika hilo limekuja kuwa mkombozi na kutatua changamoto ya maji.

Wananchi hao wamesema kuwa walikuwa wakikabiliwa na changamoto ya kutumia muda mwingi kutafuta huduma ya maji jambo ambalo kwa sasa wataepukana nalo kwa kupata mkopo wa maji usio kuwa na riba kutoka IDYDC.
Naye mwenyekiti wa Kijiji cha Mangawe Ernest Matto amesema kuwa shirika la IDYDC limewapunguzia gharama kubwa wananchi wake kuunganishiwa huduma ya maji.
Akizungumzia na Wananchi hao, Meneja wa Mradi wa kusaidia kaya maskini kupata huduma ya kuunganishiwa maji kutoka shirika la IDYDC Ndugu Castory David amesema kuwa Mkopo huo wa maji kutoka IDYDC hauna Riba hivyo wananchi watakaounganishiwa huduma hiyo ya maji wanapaswa kurejesha kwa wakati ili waweze kuwahudumia wananchi wengine wenye uhitaji.
