Nuru FM
Nuru FM
3 April 2026, 09:11

Katika operesheni hiyo, Jeshi la Polisi limefanikiwa kuokoa wahanga 75 wa mtandao huo, ambao walikuwa wakidanganywa kwa ahadi za ajira ndani na nje ya Tanzania.
Na Hafidh Ally
JESHI la Polisi mkoani Iringa limewakamata watuhumiwa wawili wanaodaiwa kuwa vinara wa mtandao wa utapeli uliokuwa ukitumia majina ya kampuni za Alliance in Motion Global na QNET kuwarubuni vijana 75 kwa ahadi ya kuwapatia ajira.
Akizungumza na waandishi wa Habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, SACP Allan Bukumbi amwataja watuhumiwa hao ni Jackson Kalu (26) mjasiliamali mkazi wa Bahi Dodoma na Michael Mfuse (32) mkazi wa Wanging’ombe mkoani Njombe walikutwa pia na gari aina ya BMW X1 iliyokuwa ikitumika kwa utapeli huo pamoja na nyaraka za kampuni ya Q-Net.
Bukumbi alisema kuwa Wahanga hao, ambao wengi wao ni vijana wenye umri kati ya miaka 20 hadi 30, wanatoka mikoa ya Dodoma, Mwanza, Lindi, Njombe, Mtwara pamoja na Mafia.
Kamanda Bukumbi amesema kuwa vijana hao 75 waliopokelewa na watuhumiwa hao na walikuwa wanachangishwa fedha zaidi shilingi laki sita mpaka milioni nne kama kiingilio kinyume na sheria.

Uchunguzi umebaini kuwa vijana hao wamekuwa wakiishi katika mazingira yasiyofaa, ambapo zaidi ya watu 10 hulazimika kulala katika chumba kimoja wakati wakisubiri kuanza shughuli hizo haramu, jambo linalokiuka sheria na kanuni za nchi.
Aidha Jeshi la Polisi mkoani Iringa kupita kamanda Bukumbi limewataka wazazi na walezi kufuatilia watoto wao kwa karibu na kufika Kituo Kikuu cha Polisi Iringa kuwatambua.
Kwa upande wao vijana waliorubuniwa na vinara hao wa utapeli wamesema kuwa waliambiwa wakijiunga na mtandao huo watapata faida endapo wataweka fedha ambazo wametajiwa.