Nuru FM
Nuru FM
15 January 2026, 12:40 pm

“Madiwani wanapaswa kuhakikisha wanasimamia ukusanyaji wa mapato na kudhibiti matumizi mabaya ya fedha ili kupeleka maendeleo kwa wananchi”
Na Fredrick Siwale
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU yawaonya Madiwani Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa wanaojipatia fedha kwa Njia ya udanganyifu.
Kauli hiyo imetolewa katika Mafunzo ya siku tatu kwa Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Madiwani wa Halmashauri ya Mji Mafinga na Afisa kutoka TAKUKURU Raymond Ngatunga na kutaka kuwe na Weledi kwa kuwa ndio dira ya Maendeleo kwa wananchi wa Mufindi.
Ngatunga amesema kuna baadhi ya Madiwani na Watumishi wa Serikali wanashiriki kutengeneza Vikundi hewa na chechefu kwa lengo ya kujipatia fedha za mikopo kwa njia ya udanganyifu.
Aidha ndugu Ngatunga amewataka madiwani kuhakikisha wanasimamia maendeleo ya Kata kikamilifu na kuwa wabunifu katika maeneo yao kwa kuibua vyanzo vipya vya mapato na pia kuwasikiliza wananchi na kutatua kero zao kwa kuwapa majibu sahihii.
Awali akitoa mada Bw. Solanus Nyimbi , Mkurugenzi wa Serikali za Mtaa Mstaafu kwa niaba ya DGL, amewashauri madiwani hao kuwa na uwajibikaji mzuri hasa katika mabaraza yao na vikao vya kamati.
Akifunga Mafunzo hayo yaliyotolewa na Wakufunzi kutoka Chuo Cha Serikali za Mtaa (Hombolo) Bi. Sifael Kivamba Afisa wa Serikali za Mitaa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ameishukuru Serikali kwa kuwaletea mafunzo hayo ambayo yatawajenga madiwani hao katika kusimamia miradi ya maendeleo ya wananchi.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bi; Fidelica Myovella ameshukuru kwa Wawezeshaji kutoa Elimu kwa Madiwani huku akitaka Mafunzo hayo yakawe Endelevu Kivitendo hata wanapokuwa kwenye Ziara madiwani hao wanatakiwa kurejea hayo Mafunzo ili kutimiza Malengo ya Serikali katika Uwajibikaji.