Nuru FM
Nuru FM
4 September 2025, 9:55 am

Mradi huo wa maji ambao uko asilimia 99 kukamilika umetajwa kuwa mkombozi kwa wananchi wa Iringa.
Na Hafidh Ally
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Maji imetekeleza ujenzi wa mradi mkubwa wa maji wa Ismani–Kilolo kwa gharama ya shilingi bilioni 9.2, mradi ambao unatarajiwa kuwanufaisha maelfu ya wananchi wa Mkoa huu.
Akizungumza katika Kijiji cha Holo, kilichofikiwa na mradi huo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Kheri James, amewataka wananchi hao kulinda miundombinu ya maji iliyojengwa na serikali kwa gharama kubwa.
Mradi huo, unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Iringa (IRUWASA), umefikia hatua ya asilimia 99 ya utekelezaji, na hadi sasa vijiji 29 vya Ismani na Kilolo vimepitiwa na mradi huo, huku zaidi ya wananchi 68,000 wakitarajiwa kunufaika moja kwa moja.

Kwa upande wao Baaadhi ya Wananchi wa eneo hilo wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuondoa adha ya maji ambapo Kabla ya mradi huo, walilazimika kutembea umbali wa hadi kilomita 5 kufuata maji, ambayo walikuwa wakishirikiana kutumia na mifugo yao.