Nuru FM

Wananchi Migoli waiomba serikali kuwavuna viboko

25 August 2025, 9:39 am

Wananchi wa Kata ya Migoli wakiwa katika mkutano wa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Kheri James na kuzungumza kero zao. Picha na Ayoub Sanga

Viboko walioko katika Bwawa la Mtera Wilaya ya Iringa wamekuwa kero kwa wananchi hao jambo linalohatarisha usalama wao.

Na Adelphina Kutika

Wananchi wa Kata ya Migoli, Wilaya ya Iringa, wameiomba Serikali kuchukua hatua za haraka kudhibiti wanyama wakali, hususan boko na mamba waliopo katika Bwawa la Mtera, wakidai kuwa wamekuwa chanzo cha vifo vya mara kwa mara kwa wakazi wa eneo hilo.

Ombi hilo limetolewa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Migoli na kuongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Kheri James ,Wakazi hao wamesema wanyama hao wamekuwa tishio kwa maisha yao, hasa wanaojihusisha na shughuli za uvuvi na kuchota maji katika bwawa hilo.

Sauti ya Wananchi

Akijibu kilio cha wananchi hao, Mkuu wa Mkoa Kheri James ameagiza Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), kwa kushirikiana na mamlaka nyingine husika, kuchukua hatua za haraka ikiwa ni pamoja na kuvuna baadhi ya wanyama hao ili kuimarisha usalama wa jamii.

Sauti ya RC Iringa Khei James
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Kheri James

Kwa upande wake Mkuu wa Hifadhi Tengefu ya Lunda-mkwabi Notikelvini Mgaya amethibitisha kutokea kwa vifo vya watu wanne kati ya mwezi Julai na Agosti, vilivyotokana na kushambuliwa na boko katika eneo la bwawa hilo.

Sauti ya Mhifadhi Mgaya

Hata hivyo Bwawa la Mtera ni chanzo muhimu cha shughuli za kiuchumi kama uvuvi, kilimo cha umwagiliaji na uzalishaji wa umeme huku likiendelea kuwa makazi ya wanyamapori hatari wakiwemo viboko na mamba, hali inayohatarisha maisha ya wananchi wanaotumia bwawa hilo.

Wavuvi katika Bwawa la Mtera