Nuru FM
Nuru FM
11 June 2025, 12:16 pm

Wateja Mkoani Iringa wametakiwa kudai risiti kila wanapofanya manunuzi, hii kudhibiti mianya ya ukwepaji kodi.
Na Adelphina Kutika
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe Peter Serukamba, amewataka wafanyabiashara wote mkoani Iringa kuacha mara moja tabia ya kutoa risiti bandia kwa wateja, akisema kuwa kitendo hicho kinasababisha upotevu mkubwa wa mapato ya serikali.
Akizungumza, katika Mkutano wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Iringa, Mheshimiwa Serukamba amesema kuwa utoaji wa risiti halali ni jukumu la kila mfanyabiashara na mchango muhimu katika kuongeza mapato ya serikali kwa ajili ya maendeleo ya taifa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chemba ya Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Kilimo (TCCIA) Mkoa wa Iringa, Bw. Hamid Mbata, amesema sekta binafsi iko tayari kushirikiana na serikali kwa karibu ili kuhakikisha kodi inakusanywa ipasavyo.
“Tunatoa ahadi yetu kama sekta binafsi kwamba tutaendelea kushirikiana bega kwa bega na serikali, Uhusiano wetu mzuri utasaidia kuhakikisha wafanyabiashara wanaelewa umuhimu wa kulipa kodi, ambayo ndiyo msingi wa maendeleo ya taifa letu,” alisema Mbata.
Katika kikao hicho wajumbe wa Baraza Hilo wameeleza baadhi ya changamoto zinazowakabili Katika sekta ya biashara,zikiwemo Sheria kandamizi Kwa wamiliki wa biashara za kulaza wageni,wakitaka zifanyiwe marekebisho ili kuendena na mazingira halisi ya biashara mkoani humo

Aidha mkutano huo wa Baraza la biashara umekuwa sehemu muhimu ya kujenga mashauriano ya karibu kati ya sekta ya umma na binafsi Kwajili ya kuimarisha uchumi wa mkoa wa Iringa na taifa Kwa ujumla.