

30 January 2025, 1:43 pm
Na Joyce Buganda
Shirika la Global Alliance for Improved Nutrition (GAIN) limegawa mbegu za maharage lishe katika shule za msingi na Sekondari Halmashauri ya Manispaa ya Iringa huku lengo ni kuhamasisha kilimo cha mazao lishe na kupambana na tatizo la utapiamlo.
Akizungumza Wakati wa zoezi la ugawaji wa maharage lishe kwa walimu wa shule zilizopo manispaa ya iringa Afisa mradi wa GAIN, Edwin Josiah amesema mbegu hizo zilizotolewa ni sehemu ya juhudi za shirika hilo katika kupambana na utapiamlo kwa kutoa msaada wa kilimo cha mazao yenye virutubisho vya kutosha kwa jamii na zoezi hilo litafanyika katika shule zilizopo Wilaya na halmashauri zote za mkoa wa Iringa.
Aidha Afisa Elimu wa elimu ya watu wazima mkoa ambae pia ni Msimamizi wa lishe Mashuleni Mwalimu Martha Lwambano amesema hayo ni maagizo ya Mkuu wa mkoa katika kuboresha afya za watoto Mashuleni hasa shule zenye maeneo walimu kupanda mazao kama maharage lishe Ili kuboresha afya za wanafunzi.
Naye Afisa lishe wa Mkoa wa Iringa, Anna Nombo amesema kuwa lengo la mkoa ni kuangalia shule ngapi zinatumia vyakula vyenye lishe ili kuhakikisha kuwa Wanafunzi wanakula vyakula vyenye virutubisho zaidi na kupata lishe inayohitajika.
Shirika la GAIN limeahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa jamii kwa kutoa msaada wa mbegu bora na elimu ya kilimo cha kisasa kwa wakulima katika mkoa wa Iringa.
MWISHO