Nuru FM
Nuru FM
2 March 2026, 5:38 pm

Kukamilika kwa skimu hiyo kunatarajiwa kuongeza eneo lenye miundombinu ya umwagiliaji kutoka ekari 4,500 zinazotegemea mifumo ya asili hadi kufikia ekari 15,000 zenye miundombinu bora na ya kudumu.
Na Hafidh Ally
Mradi wa skimu ya umwagiliaji ya Mfereji wa Mkombozi Uliopo Tarafa ya Pawaga Mkoani Iringa unatajariwa kuleta maendeleo katika sekta ya kilimo na kuongeza uzalishaji wa mazao.
Hayo yamezungumzwa na wananchi wa Tarafa ya Pawaga na kuongeza kuwa mradi huo utaondoa changamoto ya utegemezi wa mvua zisizotabirika, kuongeza tija mashambani na kuinua kipato cha kaya nyingi zinazotegemea kilimo kama chanzo kikuu cha mapato.

Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi wa mradi huo, Waziri wa Kilimo Mhe. Daniel Chongolo amesema Serikali imetenga shilingi bilioni 56 kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji nchini.
Kwa upande wake mwenyekiti wa wamiliki wa viwanda ukanda wa pawaga Lukas Ndete amesema mradi huo umekuwa na manufaa makubwa kwani maeneo ya kilimo na uzalishaji yameongezeka.
Meneja wa Umwagiliaji (NIRC), Mkoa wa Iringa, Peter Akonaay amesema mradi huo unahusisha jumla ya vijiji sita kati ya vijiji 15 vya Tarafa ya Pawaga, na ujenzi wa skimu hiyo umegawanyika katika mikataba minne inayotekelezwa na makandarasi Comfix and Engineering Ltd kwa mikataba ya LOT I na LOT II pamoja na CRJE East Africa Ltd kwa LOT III na LOT IV, ambapo jumla ya Sh56 bilioni zinatarajiwa kutumika kukamilisha miundombinu yote.
Akonaay amesema lengo kuu la mradi ni kuhakikisha upatikanaji wa maji ya uhakika kwa matumizi bora ya kilimo ili kuongeza uzalishaji wenye tija na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.