

1 February 2025, 9:47 am
Na Hafidh Ally
Halmshauri ya Mafinga Mji Mkoani Iringa imepitisha jumla ya shilingi Bilioni 31.5 katika Bajeti ya Mwaka wa fedha 2025/2026.
Akiwasilisha rasimu ya Mpango wa Bajeti ya 2025/2026 katika Baraza Madiwani, Afisa Mipango Halmashauri ya Mji Mafinga, Peter Ngussa amesema kwa mwaka wa fedha 2025/2026 Halmashauri ya Mji wa Mafinga inakadiria kutumia Jumla ya Tsh. 31.55 na kati ya fedha hizo Tsh. Bilioni 7.63 zitatokana na mapato ya ndani.
‘Waheshimiwa Madiwani kiasi cha Tsh.942,454,000.00 ni ruzuku ya matumizi mengineyo (OC), Tsh. 17,395,844,000.00ni ruzuku ya mishahara na TZS 5,581,143,000 ni ruzuku ya Miradi ya Maendeleo’ alisema Ngusa.
Ngusa amesema Halmashauri ya Mji Mafinga katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2026 imejiwekea vipaumbele vinne ambavyo ni: Kutekeleza miradi inayolenga kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato ya ndani (Own Source), Kununua maeneo ya uwekezaji, Kuendeleza ujenzi wa miradi ya kimkakati,
Kuendeleza shamba la parachichi Makalala, Kutunga na/au kuhuisha sheria ndogondogo za ukusanyaji wa mapato.,
Aidha amesema kuwa wataboresha utoaji wa huduma za jamii kwa kuendelea kutoa huduma bora kwa jamii kwa ukamilisha/kujenga miundombinu ya Sekta,Kuboresha ustawi wa wananchi kwa kuimarisha utawala bora kwa kuzingatia: demokrasia, utawala wa Sheria, haki, ushirikishwaji wa wananchi na Kuimarisha Hali ya usafi na Uhifadhi wa Mazingira katika Mji wa Mafinga.
Akichagia bajeti hiyo Mbunge wa Isalavanu Charles Makoga amesema kuwa katika bajeti hiyo ni vyema wakakamilisha miradi ya maendeleo ambayo bado hayajamaliziwa yakiwemo madarasa.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Mafinga Mheshimiwa Regnant Kivinge amewapongeza Wataalamu kutoka ofisi ya Mkurugenzi kwa Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo na Ukusanyaji wa Mapato kuongezeka mpaka kufikia Bilioni 7.6.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Mafinga Bi Fidelica Myovella amesema kuwa watahakikisha wanasimamia vyema ukusanyaji wa mapato ili waweze kufikia malengo waliyojiwekea.
Baraza la Bajeti limehudhuriwa na Katibu Tawala Wilaya ya Mufindi Ndugu Reuben Chongolo na Wataalamu kutoka Tarura na Mauwasa.
MWISHO