Jamii FM

Wananchi Makome B waiomba serikali kukamilisha ujenzi wa sekondari

2 February 2025, 12:02 pm

Mwonekano wa boma linalojengwa kwa nguvu za wananchi wa kijiji cha Makome B kwa ajili ya shule ya sekondari(Picha na Musa Mtepa)

Kijiji cha Makome B kipo umbali wa zaidi ya Kilomita 35 kutoka makao makuu ya mkoa wa Mtwara na kipo katika kata ya Mbawala,Halmashauri ya Mtwara vijijini kilichozungukwa na Milima na Mabonde pamoja na misitu asili

Na Musa Mtepa

Kutokana na changamoto ya umbali mrefu wa zaidi ya kilomita 15, wazazi na wananchi wa Kijiji cha Makome B, kata ya Mbawala, Halmashauri ya Mtwara Vijijini, wameamua kuanzisha ujenzi wa shule ya sekondari ili kuwawezesha watoto wao kupata elimu kwa urahisi na kuondoa adha wanayopata kwa kutembea umbali mrefu kila siku.

Wananchi hao wakizungumza na Jamii FM Radio na wameelezea jinsi umbali huo unavyowafanya watoto wao kuamka saa kumi alfajiri ili kujiandaa na kwenda shule ya sekondari Umoja iliyopo katika Kijiji cha Mdui.

Fatuma Abdala Fundi, mzazi mwenye mtoto anayeenda shule ya Umoja, amesema kuwa umbali huo unahatarisha mustakabali wa watoto wao, kwani wengi wao wanashindwa kumaliza elimu ya sekondari kutokana na uchovu na changamoto za usalama.

Sauti ya Fatuma Abdala Fundi Mzazi na Mwananchi wa Kijiji cha Makome B

Wananchi wengine, Hassani Chihako na Ahmadi Mnyamba, wameongeza kuwa umbali mrefu unakwamisha wasichana kumaliza elimu ya sekondari kwa usalama, na kuna hatari ya kukutana na vishawishi vinavyoweza kuathiri masomo yao, ikiwemo kupata ujauzito na kuacha shule.

Sauti ya Hassani Chihapo na Ahamadi Mnyamba wakazi wa Makome B

Kutokana na changamoto hiyo, wananchi wa Kijiji cha Makome B wameanzisha ujenzi wa shule ya sekondari kwa kujenga boma lenye vyumba vitatu na ofisi moja ya walimu, ambayo tayari imefikia hatua ya kufunga linta. Hata hivyo, wanahitaji msaada zaidi kutoka kwa serikali na wadau ili kukamilisha ujenzi huo na kuhakikisha watoto wanapata elimu bora.

Sauti ya 3 wananchi wa Makome B

Mwenyekiti wa serikali ya Kijiji cha Makome B, Bakari Mkanjalanga, amekiri kuwepo kwa changamoto ya umbali mrefu na kuelezea juhudi zinazofanywa na wananchi kujenga shule hiyo kwa kuchangia shilingi 12,000 kwa kila mwananchi.

Sauti ya Bakari Salumu Mkanjalanga mwenyekiti wa Kijiji cha Makome B

Hata hivyo, ameeleza kuwa hapo awali walikubaliana na  Wananchi kukatwa kiasi kidogo cha fedha kupitia zao la korosho ili kufanikisha ujenzi wa shule hiyo ila hali imekuwa tofuati na matarajio , kwani hadi kufikia Januari 30, 2025, fedha za wananchi hazijapatikana kutoka kwa chama cha ushirika cha Umoja, kutokana na kutokana na mkanganyiko na utata wa taarifa za fedha.

Sauti ya Bakari Salumu Mkanjalanga mwenyekiti wa Makome B

Wananchi wa Kijiji cha Makome B wanaendelea kuomba msaada na ushirikiano kutoka kwa serikali na wadau wengine ili kuhakikisha ujenzi wa shule unakamilika na kutoa fursa kwa watoto wa kijiji hicho kupata elimu kwa usalama zaidi.