Mpanda FM
Mpanda FM
27 March 2026, 12:55 pm

“Wananchi wanaendelea kupata elimu ya masuala ya ukatili wa kijinsia pamoja na haki za binadamu na elimu ya ujasiliamali kwa vijana ili waweze kujihimarisha kiuchumi.”
Na Anna Milanzi- Katavi
Taasisi isiyo ya kiserikali ya Tuelimike iliyopo mkoani Katavi imefanya mkutano wa kuhitimisha mwaka wa mradi 2025-2026.
Katika mkutano huo uliofanyika katika halmashauri ya Nsimbo wanufaika wa mafunzo ya elimu ya usawa wa kijinsia na haki za binadamu wameeleza namna ambavyo wanatoa elimu kwa jamii kuhusu vitendo vya ukatili wa kijinsia na haki za binadamu.
Awali akisoma Taarifa ya utekelezaji wa mradi huo Afisa utawala fedha Alkado Kalmalando amesema mafunzo yaliyotolewa ni ya haki za binadamu,usawa wa kijinsia pamoja na ujasiriamali ambapo mafunzi hayo yametolewa kwa uwakilishi wa kila makundi ikiwemo vijana viongozi wa dini ,wazee maarufu, watu wenye ulemavu na wengine wengi.
Mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo Douglas Mwaisaka amesema licha ya mafanikio yaliyopo ipo changamoto ya vijana wanaowapatia mafunzo hayo kutokufanyia kazi mafunzo waliyopatiwa kutokana na sababu mbalimbali.
Mgeni rasmi katika mkutano huo ambaye ni afisa maendeleo ya jamii halmashauri ya Nsimbo Alex Magele amesema ili kuondokana na changamoto za vijana kupatiwa mafunzo na kushindwa kuendeleza wanatakiwa kuhamasishwa kujiunga katika vikundi ili waweze kupatiwa mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na serikali
Elimu iliyotolewa na asasi ya tuelimike kwa mwaka wa mradi 2025-2026 imewafikia jumla ya wanufaika 180 ambao nao wamekuwa wakitoa elimu kwa wananchi wengine. Mradi huo unafadhiliwa na serikali ya Canada.