Mpanda FM
Mpanda FM
24 February 2026, 1:25 pm

Picha na mtandao mwananchi
“Tukio hili limetushtua sana huu ni ukatili”
Na Anna Mhina
Wakazi wa mtaa wa Tulieni, kata ya Nsemulwa, Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi, wamepatwa na mshtuko kufuatia kukutwa kwa mwili wa msichana mmoja ndani ya shimo la kufyatulia tofali.
Msichana huyo, ambaye jina lake limehifadhiwa, anakadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 17 hadi 19, Mwili wake uligunduliwa asubuhi ya kuamkia Februari 23, 2026 katika shimo lililopo jirani na nyumbani kwao.
Akizungumza na Mpanda Radio FM, msemaji wa familia amesema kuwa siku ya Jumapili February 22 mwaka 2026 majira ya saa nne usiku, binti huyo alitoka nje ya nyumba baada ya kupigiwa simu mara kadhaa na hakurejea tena.
Mwenyekiti wa mtaa wa Tulieni, Hussein Kasomela, amesema alipokea taarifa za tukio hilo na kuchukua hatua za kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Kwa upande wake, Diwani wa kata ya Nsemulwa, Alex Ngereza, ametoa pole kwa familia na kuwataka wananchi kushirikiana na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa zitakazosaidia katika uchunguzi.
Baadhi ya wakazi wa eneo hilo wameeleza kusikitishwa na tukio hilo na kuomba mamlaka husika kuchukua hatua za haraka ili kubaini kilichotokea.
Juhudi za kuwapata viongozi wa Jeshi la Polisi mkoani Katavi ili kutoa taarifa rasmi kuhusu tukio hilo zinaendelea, na tutawaletea taarifa zaidi pindi zitakapopatikana.