Mpanda FM

Wamiliki wa viwanda vya kubangua karanga Mpanda hotel watakiwa kuhama

24 June 2024, 7:02 pm

Takataka zilizotokana na kazi ya ubanguaji karanga katika eneo la mpanda hotel na kuleta kero kwa wakazi wa maeneo hayo.Picha na Samwel Mbugi

Mashine zilizopo maeneo hayo zinazalisha taka nyingi ambazo zinasababisha uchafuzi wa mazingira na kupelekea manispaa kuwa chafu

Na Samweli Mbugi – Katavi

Kufuatia malalamiko ya wananchi wa kata ya Mpanda Hotel mkoa wa Katavi juu ya kero ya viwanda vya kubangulia karanga kusababisha uchafu katika makazi yao pamoja na ugonjwa wa mafua, Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Jamila Yusuph ametoa maagizo kwa wamiliki kuhama eneo hilo na kuzoa takataka zote.

Hayo yamesemwa wakati wa ukaguzi wa viwanda hivyo na kubaini kuwa viwanda hivyo vipo ndani ya makazi ya watu, ambapo amesema serikali imewavumilia kutokana na udhaifu uliojitokeza kipindi cha nyuma.

Hayo yanajiri ikiwa ni wiki moja imepita tangu Mpanda Radio FM iripoti taarifa juu ya wananchi wa kata ya Mpanda Hotel kulalamikia viwanda vilivyopo eneo hilo na uchafu kutokutolewa kwa wakati na hivyo kusababisha  kuibuka kwa ugonjwa wa mafua.

Sauti ya DC Jamila Yusuph akitoa maagizo ya kuzolewa kwa taka hizo na kuhama katika eneo hilo

Kwa upande wake Mkurugenzi manispaa ya Mpanda Sophia Kumbuli amewataka wamiliki wa viwanda hivyo kuziondoa takataka zote na sio kuchoma kwani uchomaji unapelekea uchafuzi wa hali ya hewa.

Sauti ya mkurugenzi mtendaji manispaa ya Mpanda Sophia Kumbuli akieleza namna hatua zilivyochukuliwa na kuwataka kuzoa takataka hizo

Kwa upande wake Afisa Afya Manispaa ya Mpanda Erick Kisaka ametoa taarifa juu ya usafi wa kata ya Mpanda Hotel na Makanyagio ambapo amesema kuwa mashine zilizopo maeneo hayo zinazalisha taka nyingi ambazo zinasababisha uchafuzi wa mazingira na kupelekea manispaa kuwa chafu.

Sauti ya Afisa Afya Erick Kisaka akitoa taarifa juu ya mwenendo wa usafi katika eneo hilo

Wito umetolewa kwa wamiliki wa viwanda hivyo kuwa jambo hilo lisijirudie tena na endapo itabainika makosa hayo kujirudia serikali haitasita kuwachukulia hatua za kisheria.