Jamii FM

Wanafunzi Mtwara waaswa kutojihusisha na mapenzi wakiwa shuleni

7 March 2025, 07:57 am

Baadhi ya Wanafunzi wa shule ya Sekondari Chuno wakisikiliza kwa makini Nasaha za Bi Zainabu Kibunju ,kungwi kutoka Mtwara mjini (Picha na Musa Mtepa)

Haya yamejiri kwenye tamasha la michezo lililoandaliwa na shirika la Sports Development Aid likihusisha wanafunzi wa shule za sekondari za Likombe na Chuno zilizopo Manispaa ya Mtwara Mkindani likiwa na lengo la kufikisha ujumbe kupitia michezo wa kuepukana na ukatili na usawa wa kjinsia katika jamii

Na Musa Mtepa

Wanafunzi Mtwara wameaswa kutojihusisha katika mapenzi wakiwa bado masomoni ili kufikia malengo yao ya kielimu.

Akizungumza March 4 , 2025 kwenye tamasha la michezo lililoandaliwa na shirika la Michezo la Sports Development Aid(SDA) kwa kushirikiana na TASA na SSDM, Bi Zainabu Kibunju, kungwi wa mjini Mtwara, amewashauri wanafunzi wa kike na wa kiume kuepuka kujihusisha kimapenzi wakiwa mashuleni, kwani kufanya hivyo kunaweza kuathiri uwezo wao wa kufanya vizuri katika masomo.

Aidha, Bi Kibunju amewataka wanafunzi kujiepusha na mahusiano ya kimapenzi na walimu wao, hususan walimu wa field, ambao kwa baadhi ya tafiti zisizo rasmi zimeonyesha kuwa wamekuwa wakijihusisha kimapenzi na wanafunzi, jambo linaloleta madhara kama kupata ujauzito na kukatisha masomo.

Sauti ya Bi Zainabu Kibunju Kungwi kutoka mjini Mtwara
Kungwi Bi Zainabu Kibunju akitoa nasaha zake mbele ya wanafunzi wa shule ya sekondari Chuno na Likombe (Picha na Musa Mtepa)

Paulina Lidasi, mwanafunzi wa Kidato cha Tatu kutoka Shule ya Sekondari Likombe, amekiri changamoto za walimu na bodaboda kuwa na mahusiano kimapenzi na wanafunzi na kuahidi kukabiliana na changamoto hizo kwa njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na kushirikisha viongozi wa kiserikali.

Sauti ya Paulina Lidasi Mwanafunzi wa shule ya sekondari Likombe

Maila Bashiru, mwanafunzi kutoka Shule ya Sekondari Chuno, amesema kwamba wasichana wamekuwa wakikumbana na changamoto nyingi kutoka kwa wanaume, ikiwa ni pamoja na kupewa fedha na chips ikiwa njia ya kuwashawishi kuingia katika mahusiano ya kimapenzi na kueleza  kuwa kupitia mafunzo ya Bi Kibunju, wataweza kujiepusha na changamoto hizo.

Sauti ya Maila Bashiru Sadi Mwanafunzi wa Chuno Sekondari

Kwa upande mwingine, Ali Mvita, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Likombe, amezungumzia kuhusu umuhimu wa kujua malengo yake na jinsi ya kuyafikia huku akisisitiza  umuhimu wa jamii na serikali kulinda watoto wa kiume dhidi ya vitendo vya ubakaji.

Sauti ya Ali Mvita Mwanafunzi wa shule ya sekondari Likombe