Jamii FM

Wananchi Makome B: Maji yalitoka dakika tano tu

7 January 2026, 19:27 pm

Tanki la maji liliojengwa katika kijiji cha Makome B ambao ni mradi unaohusisha vijiji viwili vya Makome A na B ambao ujenzi wake umefikia asilimia 65(Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Makome B wameiomba Serikali kupitia RUWASA kukamilisha mradi wa maji uliosimama ili kumaliza uhaba wa maji safi unaosababisha magonjwa na changamoto za kijamii.

Na Musa Mtepa

Wananchi wa kijiji cha Makome B kilichopo kata ya Mbawala,Halmashauri ya Mtwara vijijini, Mkoani Mtwara wameiomba Serikali kupitia Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kukamilisha mradi wa maji unaojengwa katika kijiji hicho ili kuondokana na adha ya uhaba wa maji safi na salama inayowakabili.

Wakizungumza na waandishi wa habari January 6 ,2026 wananchi hao wamesema kuwa kutokana na kukosekana kwa maji safi na salama, wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali za kiafya na kijamii, hali inayotokana na matumizi ya vyanzo vya maji vya asili ambavyo si salama kwa matumizi ya binadamu.

Wakazi wa kijiji hicho, Mwanahamisi Mitole na Sinani Kibwana, wamesema tatizo la maji limesababisha kuongezeka kwa magonjwa ya tumbo, hatari ya kushambuliwa na wanyama wakali pamoja na migogoro ya kifamilia, hali inayohatarisha ndoa zao. Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wameomba wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kukamilisha mradi wa maji uliosimama katika kijiji hicho.

Sauti ya Mwanahamisi Mitole na Sinana Kibwana, wakazi wa Makome B
Wananchi wa kijiji cha Makome B wakiteka Maji katika kisima cha asili kilichopo kijijini hapo(Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B, Ndugu Salumu Liwingu, amekiri kuwa hali ya upatikanaji wa maji safi na salama katika kijiji hicho ni mbaya, kwani wananchi wanategemea maji yanayotiririka kutoka maeneo mbalimbali ambayo si salama, hali inayochangia wananchi kupata magonjwa ya tumbo mara kwa mara.

Sauti ya Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B
Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B(Picha na Musa Mtepa)

Akizungumzia mradi wa maji unaojengwa kijijini hapo, Mwenyekiti huyo amesema mradi huo umeingia mwaka wa tatu tangu kuanza kwake. Ameeleza kuwa mradi huo ulizinduliwa rasmi mwaka 2024 wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru, lakini maji yalitoka kwa takribani dakika tano pekee na tangu hapo hakuna maji yaliyowahi kutoka tena.

Sauti ya Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Mtwara, Abdulaziz Hemedi, amesema mradi wa maji wa Makome umefikia asilimia 65 ya utekelezaji, huku asilimia 41 ya fedha za mradi zikiwa tayari zimeshalipwa kwa mkandarasi. Amesema changamoto mbalimbali zimejitokeza na kusababisha mradi huo kushindwa kutoa huduma ya maji kwa wananchi wa Makome A na B, hali iliyopelekea RUWASA kufikiria kuvunja mkataba na mkandarasi husika.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara
Mwonekano wa kisima cha asili cha maji kinachotumiwa na wananchi wa Makome B kunywa,kuoshea na kuogea(Picha na Musa Mtepa)

Aidha, amesema mkataba wa ujenzi na ukamilishaji wa mradi huo ulitarajiwa kukamilika mwezi Novemba 2025, na kufikia wakati wanapofikiria kuvunja mkataba, utekelezaji ulikuwa umefikia asilimia 65.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara
Mwonekano wa baadhi ya Bomba zilizo telekezwa porini baada ya mkandarasi wa kutokamilisha ujenzi wa mradio huo(Picha na Musa Mtepa)

Hata hivyo, Kaimu Meneja huyo amesema pamoja na mchakato wa kuvunja mkataba na kumpata mkandarasi mpya wa kukamilisha mradi huo, wananchi wa vijiji vya Makome A na B wanatarajiwa kupata huduma ya maji safi na salama ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Wizara ya Maji na ofisi mbalimbali za Serikali, hadi kufikia mwezi Julai 2025 upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika maeneo ya vijijini umefikia asilimia 83 na Sera ya Taifa ya Maji ikisisitiza upatikanaji endelevu wa maji safi na salama kwa kuhusisha jamii, sekta binafsi pamoja na kulinda rasilimali za maji ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wananchi wote wa vijijini.

Wananchi wa kijiji cha Makome B wakiwa njiani kuelekea Nyumbani wakitokea Kisimani kuteka maji(Picha na Musa Mtepa)