Mpanda FM
Mpanda FM
11 March 2026, 4:37 pm

“Ni kosa kisheria kutotoa taarifa pindi bomba linapopasuka”
Na Anna Mhina
Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Mpanda hotel uliopo manispaa ya Mpanda mkoani Katavi wameiomba mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira (MUWASA) kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa kutoa taarifa pindi wanapoona bomba la maji limepasuka.
Wakizungumza na Mpanda radio FM wananchi hao wamesema kuwa ukosefu wa elimu unapelekea mamlaka kupata hasara huku wengine wakichukulia kama fursa ya kupata maji kwa urahisi kutokana na changamoto ya upatikanaji wa maji.
Kwa upande wake kaimu mkurugenzi wa mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira (MUWASA) ambaye pia ni meneja usambazaji maji Mpanda mhandisi Philipo Pagati amesema ni kosa kisheria kwa mwananchi kutotoa taarifa na kueleza mikakati yao kama mamalaka ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu katika kila mtaa.
Hata hivyo tatizo la ukosefu wa maji safi na salama limekuwa likiwakabili wananchi katika maeneo mbalimbali Katavi ambapo wengine hulazimika kutembea umbali mrefu au hata kununua maji ili kukidhi mahitaji yao ya kila siku.