Jamii FM

Mwenge wa uhuru wapongeza mradi wa vijana Mtwara Mikindani

26 May 2025, 14:36 pm

Kiongozi mkuu wa wakimbiza mwenge wa uhuru 2025 Ndugu Ismail Ali Ussi akisalimiana na mkuu wa wilaya ya Mtwara Abdala Mwaipaya baada ya kukata utepe wa kukubali kutembelea mradi wa uzalishaji malighafi za ujenzi kutoka kikundi cha vijana ujenzi enterpreneur kilichopo Mbae Mashariki Manispaa ya Mtwara Mikindani (Picha na Musa Mtepa)

Ni zaidi ya kilomita 40 mwenge umekimbizwa katika halmashauri ya Mtwara Mikindani huku ikipita katika miradi sita ya maendeleo ambapo yote mkimbiza Mwenge wa uhuru kitafa ameridhia utekelezaji wake

Na Musa Mtepa 

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Ndugu Ismail Ali Ussi, Mei 25, 2025, ametembelea na kukipongeza Kikundi cha Vijana cha Wajenzi Entrepreneur kilichopo Mbae Mashariki, Manispaa ya Mtwara Mikindani, ambacho kinajishughulisha na uzalishaji na uuzaji wa malighafi za ujenzi.

Katika hotuba yake, Ndugu Ussi ameeleza kuridhishwa kwake na jinsi kikundi hicho kilivyotumia vyema mkopo wa asilimia 10 kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani kupitia mapato ya ndani, kiasi cha Shilingi Milioni 32.7.

Sauti ya 1: Ismail Ali Ussi, Mkimbiza Mkuu wa Mwenge wa Uhuru Kitaifa)

Aidha, ameipongeza Halmashauri hiyo pamoja na kikundi hicho kwa hatua yao ya kusajiliwa katika mfumo wa kidigitali wa NeST, hatua ambayo itawawezesha kushiriki kikamilifu kwenye zabuni na tenda zinazotolewa na serikali, akibainisha kuwa mfumo huo unathamini usalama na unamilikiwa na serikali tofauti na mfumo wa awali.

Sauti ya 2: Ismail Ali Ussi Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa uhuru kitaifa

Kwa niaba ya Mwenyekiti wa kikundi, Ramadhani Ismail Mmogo amewasilisha taarifa ya mradi, akieleza kuwa ulianzishwa tarehe 1 Julai 2023 ukiwa na wanachama sita (wanaume wanne na wanawake wawili), na ulilenga kuwainua kiuchumi vijana kupitia biashara ya malighafi za ujenzi. Mradi huo umegharimu jumla ya Shilingi Milioni 39.7.

Sauti ya Ramadhani Mmogo, Msoma Taarifa ya Kikundi
Vijana wanakikundi cha vijana ujenzi Enterpreneur wakiwa katika uchanganyaji wa udongo na saruji tayari kwa ajili ya uzalishaji wa tofali (Picha na Musa Mtepa)

Ameongeza kuwa mikakati ya kikundi ni pamoja na kuwa taasisi kubwa inayotoa bidhaa bora za ujenzi kutoa ajira kwa wanawake na vijana,kupata eneo la kudumu kwa ajili ya ofisi ya kikundi.

Sauti ya Ramadhani Mmogo, Msoma Taarifa ya Kikundi
Akina mama wanakikundi wa vijana ujenzi Enterpreneur Group wakiwa katika uzalishaji wa kokoto (Picha na Musa Mtepa)

Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2025 katika Manispaa ya Mtwara Mikindani zimepitia miradi sita ya maendeleo, ambayo ni kikundi cha Vijana Mbae Mashariki,Jengo la OPD Mtawanya,Shule ya Sekondari Tandika,ofisi ya Mtaa wa Majengo.mradi wa Maji – Mtaa wa Mwera, na kituo cha Redio cha HFM.