

21 March 2025, 15:39 pm
Mwaka 2025 Tanzania inatarajia kufanya uchaguzi mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais ambapo kupitia mafunzo hayo yatawawezesha waandishi wa habari kupitia vipindi vyao kushawishi wanawake kuingia katika kinyanyiro cha uchaguzi.
Na Mwanaidi Kopakopa
Leo tarehe 21 Machi 2025, Chama cha Wanahabari Wanawake (TAMWA) kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Vyombo vya Habari Finland VIKES, wameendesha mafunzo kwa waandishi wa habari kuhusu jinsi ya kuwahamasisha wanawake kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka huu 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari, mhariri wa jukwaa la kupashana habari Radio TADIO, Bw. Hilali Alexander Ruhundwa, amewasisitiza waandishi hao kuandaa vipindi vitakavyowapa motisha wanawake ili waweze kujitokeza kuwania nafasi za uongozi.
Amesisitiza kuwa ni muhimu kwa waandishi wa habari kutengeneza mazingira ya kijasiri ambayo yatawafanya wanawake kuwa na ujasiri wa kugombea.
Kwa upande mwingine, Meneja wa Mikakati na Mipango wa TAMWA, Bi. Sylvia Doulinye, ameeleza kuwa mafunzo hayo yatasaidia waandishi wa habari kuwawezesha wanawake kwa kuwapa maarifa na mbinu za kujiinua kisiasa.
Amesema kuwa kupitia elimu hii, wanawake wataweza kupata maarifa yatakayowawezesha kushiriki katika mchakato wa uchaguzi na kufanikiwa kugombea nafasi za uongozi.
Kwa upande wake Mariamu Kasawa ameshukuru kupata mafunzo hayo kwani yatawasaidia katika kuandaa vipindi vitakavyosaidia katika kuhamasisha na kuwafikia wanawake kuelekea uchaguzi mkuu
Mafunzo hayo, yaliyofanyikia jijini Dodoma, yameandaliwa na TAMWA kwa kushirikiana na VIKES.