Jamii FM
Jamii FM
18 May 2025, 15:35 pm

“Mradi huu utatusadia kuondokana na kero tunazopata kwani hapo awali maji ya kutawaza tulikuwa tunaenda kuchota Bondeni Mandawa hivyo huu mradi ni suluhisho tosha la changamoto hii”
Na Musa Mtepa
Waumini wa dini ya Kiislamu wanaoswali katika Msikiti wa Nuru Islamia uliopo Kata ya Naliendele, Manispaa ya Mtwara Mikindani, wameishukuru kampuni ya Water for Life na Sherazade kwa kuwachimbia na kuwajengea kisima cha maji katika msikiti huo.
Waumini hao wamesema hapo awali walikuwa wakilazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji, licha ya kuwepo kwa mtandao wa maji kutoka MTUWASA, ambao haukuwa na uhakika wa upatikanaji wake.
Akizungumza kwa niaba ya waumini, Mzee Selemani Lenga ambaye ni mweka hazina wa msikiti huo, amesema kisima hicho kitakuwa msaada mkubwa kwa wakazi wa eneo hilo lenye watu zaidi ya elfu kumi na tatu.

Mzee Lenga ameongeza kuwa ujenzi wa kisima hicho umegharimu zaidi ya shilingi milioni 18, huku akieleza kuwa lengo ni kuhakikisha mradi huo unakuwa endelevu na wenye manufaa kwa jamii.
Nao baadhi ya viongozi wa msikiti wameeleza kuwa kisima hicho kimekuja wakati muafaka, kwani kimepunguza gharama na usumbufu wa kutafuta maji kwa waumin

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Water for Life, Mohamedi N’didi, amesema kampuni yake imeamua kusaidia baada ya kuona juhudi za waumini waliokuwa wameanzisha mchakato wa kuchimba kisima hicho kwa michango yao na huku akiwataka mradio huo usiwe chanzo cha fitna na kufarakanisha waumini.

Mradi huo wa kisima unatarajiwa kunufaisha si tu waumini wa msikiti huo, bali pia wakazi wa maeneo ya jirani, kwa kuwapatia huduma ya maji safi na salama kwa matumizi ya kila siku.
