Jamii FM

DC Mtwara awataka wajasiriamali kuwajibika kwa mikopo

16 November 2025, 10:08 am

DC Mwaipaya akizungumza na wajasiliamali na wafanyabiashara wa soko kuu mtwara wakati wa mkutano wa WABISOKO katika viwanja vya Mashujaa jana November 15,2025 (Picha na Musa Mtepa)

Mkuu wa Wilaya Abdala Mwaipaya amesisitiza uwajibikaji huo kwenye mkutano wa WABISOKO na kuwapongeza wafanyabiashara kwa kudumisha amani na kuwasilisha changamoto zao kwa utulivu. Makamu Mwenyekiti Rashidi Johana amewasilisha maendeleo na changamoto za ushirika.

Na Musa Mtepa

Wajasiriamali wametakiwa kutimiza wajibu wao katika kufanikisha upatikanaji na urejeshaji wa mikopo inayotolewa na serikali kupitia benki washirika, ili kuwezesha watu wengine kunufaika na huduma hiyo.

Kauli hiyo imetolewa Novemba 15, 2025 na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdala Mwaipaya, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Ushirika wa Wafanyabiashara wa Soko Kuu Mtwara (WABISOKO) uliofanyika katika viwanja vya Mashujaa, Manispaa ya Mtwara–Mikindani.

Mwaipaya amesema kuwa serikali inatekeleza wajibu wake, lakini ni muhimu kwa wajasiriamali kama walengwa wa mikopo hiyo kuhakikisha wanatimiza masharti na vigezo vinavyohitajika ili kupata na kurejesha mikopo ipasavyo.

Sauti ya 1: Abdala Mwaipaya, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara

Aidha, DC Mwaipaya ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla kwa kudumisha amani na utulivu katika kipindi cha uchaguzi mkuu uliopita. Pia amewapongeza viongozi wa jumuia hiyo kwa kuwa watulivu na kuwasilisha changamoto zao bila kuanzisha vurugu au fujo.

Sauti ya 2: Abdala Mwaipaya, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Ushirika wa Wafanyabiashara wa Soko Kuu Mtwara (WABISOKO), Bw. Rashidi Issa Johana, amesema kuwa dhamira kuu ya mkutano huo ni kuwapa wanachama taarifa ya maendeleo tangu viongozi wa sasa walipochukua madaraka, pamoja na changamoto na mafanikio yaliyopatikana.

Sauti ya Rashidi Issa Johana, Makamu Mwenyekiti WABISOKO
Wajasiliamali wakiwa kwenye mkutano wa WABISOKO (Picha na Musa Mtepa)