Jamii FM

EWURA yatoa mafunzo kwa wadau wa huduma za  nishati na maji Mtwara

15 March 2025, 10:59 am

Bw John Luguzya , Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu ofisi ya mkuu wa mkoa akifungua mafunzo ya siku moja kwa wadau wa Huduma za Nishati na Maji (Picha na Musa Mtepa)

Haya ni mafunzo ya siku moja yaliyohusisha watendaji wa mitaa,viongozi wa dini,wadau na watumiaji wa huduma za maji na Nishati wanaopatikana Manispaa ya Mtwara Mikindani

Na Musa Mtepa

Mamlaka ya Uthibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendesha mafunzo kwa watendaji wa mitaa na wadau mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kujenga uelewa kuhusu ushirikiano na mamlaka, pamoja na utambuzi wa sheria za mtumiaji na mtoa huduma.

Mafunzo hayo yamefanyika tarehe 14 Machi 2025 katika Hoteli ya Lavilla Nouvelle, iliyopo katika Manispaa ya Mtwara Mikindani.

Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mtwara, Bw. John Luguzya, Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, amewapongeza EWURA kwa kuandaa mafunzo hayo, akieleza kuwa yataongeza uelewa wa masuala ya kiuthibiti, hasa katika sekta za umeme na maji.

Sauti ya 1 John Luguzya katibu tawala msaidizi,usimamizi wa rasilimali watu mkoa wa Mtwara

Bw. Luguzya amefafanua kuwa, moja ya majukumu ya EWURA ni kuhakikisha huduma za umeme na maji zinapatikana kwa uhakika ili ziweze kuchangia katika ustawi wa uchumi wa nchi.

Sauti ya 2 John Luguzya katibu tawala msaidizi,usimamizi wa rasilimali watu mkoa wa Mtwara

Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Wilfred Mwakalosi, amesema kuwa mafunzo hayo yatasaidia washiriki kuwa katika nafasi nzuri ya kutoa ushauri kwa wananchi kuhusu changamoto zinazojitokeza katika maeneo yao.

Sauti ya Wilfred Mwakalosi Meneja wa EWURA kanda ya Mashariki.

Nicolous Mvukie, Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Ligula, pamoja na Shehe Mohamed Lidonge, wameeleza kuwa mafunzo hayo yamewaongezea uelewa mkubwa kuhusu masuala ya bili za maji, matumizi ya umeme, na jinsi ya kuchukua hatua pindi wanapokutana na changamoto.

Aidha wamesisitiza kuwa, EWURA inapaswa kuendelea kutoa elimu hiyo kwa wananchi wa chini kupitia mikutano ya vijiji na mitaa ili kuongeza uelewa juu ya malalamiko yaliyopo katika jamii kuhusu utumiaji wa maji na umeme.

Sauti ya Nicolous Mvukie na shehe Mohamed Lidonge washiriki wa mafunzo.