Jamii FM
Jamii FM
13 April 2026, 12:24

Wananchi wa kijiji cha Mnuyo mkoani Mtwara wamelalamikia mashambulizi ya viboko mashambani, wakiiomba serikali kuchukua hatua za haraka kuwalinda na kuzuia hatari ya baa la njaa.
Na Musa Mtepa
Wananchi wa Kijiji cha Mnuyo, kata ya Msimbati, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara, mkoani Mtwara, wameiomba serikali kupitia mamlaka zinazohusika na wanyamapori kufika kijijini hapo ili kuwaondolea changamoto ya wanyama aina ya viboko wanaoshambulia mashamba yao ya mpunga.
Wakizungumza na Jamii FM Redio Aprili 10,2026, wananchi hao wamesema kuwa katika siku za hivi karibuni wamekuwa wakikumbwa na changamoto kubwa ya viboko kuvamia mashamba yao ya mpunga nyakati za usiku, hali inayowatishia baa la njaa siku za usoni.

Aidha, wananchi hao wameiomba serikali kuwasaidia kwa haraka kutatua changamoto hiyo, ambayo imekuwa kubwa kwao kiasi cha baadhi yao kukata tamaa ya kuendelea na shughuli za kilimo kutokana na uwepo wa wanyama hao.

Kwa upande wake, mwenyekiti wa Kijiji cha Mnuyo, Yusuf Salumu, amekiri kupokea taarifa za uwepo wa wanyama hao katika eneo hilo, akisema tayari amezifikisha katika Halmashauri ya Wilaya kwa ajili ya hatua zaidi.
Aidha, mwenyekiti huyo amesema viboko hao wanaotoka Mto Ruvuma wameshashambulia mashamba 15 ya wakulima wa kijiji hicho, huku akiomba mamlaka zinazohusika na wanyamapori kuchukua hatua za haraka kuwaondoa wanyama hao.