Jamii FM
Jamii FM
4 February 2026, 06:50 am

Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara imesema inaendelea kuimarisha uwezo wake ili kuhakikisha utoaji wa haki kwa wakati kama sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Kauli hiyo imetolewa wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika Mtwara.
Na Musa Mtepa
Katika kutekeleza mipango ya maendeleo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Mahakama kwa kushirikiana na Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha uwezo wake ili kusimamia utoaji wa haki kwa wakati kwa taasisi, mashirika na wananchi nchini.
Hayo yameelezwa Februari 2, 2026 na Mheshimiwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara, Edwin Kakolaki, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini yaliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara.

Mheshimiwa Jaji Kakolaki amesema kuwa katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, muhimili wa Mahakama una nafasi muhimu katika kujenga taifa lenye haki, amani, usalama na utulivu kwa kujenga mazingira salama ya kisiasa, kijamii na kiuchumi.

Aidha, Jaji Kakolaki amesema Mahakama imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika matumizi ya teknolojia, hatua inayochangia kuongeza ufanisi na kasi ya utendaji kazi ikilinganishwa na miaka ya nyuma, jambo linalosaidia wananchi kupata haki kwa wakati.

Akitoa salamu za maadhimisho hayo, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mkoa wa Mtwara, Lightness Kikao, amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo imebeba uzito mkubwa kwa kuwa inaakisi ukweli kwamba hakuna maendeleo ya kweli bila uwepo wa haki, utawala wa sheria na misingi ya utawala bora.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrik Sawala, ambaye alikuwa mgeni maalumu katika maadhimisho hayo, amesema utoaji wa haki kwa wakati kwa wananchi utadumisha amani na utulivu katika mkoa wa Mtwara na taifa kwa ujumla, hali itakayowapa wananchi fursa ya kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo kwa amani.
