Mpanda FM
Mpanda FM
6 April 2026, 1:35 pm

“Naomba nisisitize msiamini katika uvumi”
Na Benny Gadau
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko amekemea vikali vitendo vya wananchi kujichukulia sheria mkononi na kudhuru wengine kutokana na taarifa zisizo na ukweli, akisisitiza kuwa vitendo vya aina hiyo pamoja na kueneza uzushi havitavumiliwa na serikali.
Mrindoko ametoa kauli hiyo jumapili Aprili 5, 2026, mara baada ya kushiriki ibada ya Pasaka katika Kanisa la Anglikana lililopo kata ya Makanyagio manispaa ya Mpanda.
Amesema baadhi ya taarifa zinazosambazwa mitandaoni na katika jamii hususani zile zenye mwelekeo wa kishirikina na uzushi zimekuwa zikichochea taharuki, hofu na migogoro isiyo ya lazima.
Ameongeza kuwa vyombo vya dola vitaendelea kuwachukulia hatua kali za kisheria wote watakaobainika kuhusika katika uenezaji wa taarifa za upotoshaji na uzushi unaosababisha hofu na kuvuruga utulivu wa jamii.
Mkuu huyo wa mkoa amewahakikishia wananchi kuwa hali ya usalama katika mkoa wa Katavi ni shwari na kuwataka kuendelea na shughuli zao za kila siku bila hofu yoyote.