Jamii FM

Wazazi mkoani Mtwara wahimizwa kuweka kipaumbele elimu kwa wenye ulemavu

29 January 2026, 18:30 pm

Mkurugenzi wa MERODI Frances Chiwango akiwa na wadau wa elimu wakizungumzia umuhimu wa elimu kwa wenye ulemavu(Picha na Musa Mtepa)

Wazazi na walezi mkoani Mtwara wametakiwa kuwapeleka shule watoto wenye ulemavu katika kipindi hiki cha uandikishaji wa Elimu ya Awali na Msingi. Wito huo umetolewa na MERODI kupitia Jamii FM, ikisisitiza elimu jumuishi, ushirikiano wa jamii na msaada wa serikali kwa wazazi wa watoto wenye ulemavu

Na Musa Mtepa

Wazazi na walezi mkoani Mtwara wametakiwa kuweka kipaumbele katika elimu kwa watoto wenye ulemavu kwa kuhakikisha wanawaandikisha katika kipindi hiki cha uandikishaji wa Elimu ya Awali na Msingi kinachoendelea kote nchini.

Wito huo umetolewa leo Januari 29, 2026 na Frances Chiwango, Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi isiyo ya kiserikali inayojihusisha na watu wenye ulemavu mkoani Mtwara ya Mtwara Economic Rights Organization for Disabled (MERODI), alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Dira ya Asubuhi kinachorushwa na Jamii FM Radio.

Akizungumza katika kipindi hicho, Chiwango amesema licha ya kuwepo kwa mwamko kwa baadhi ya wazazi na walezi ikilinganishwa na miaka ya nyuma, bado juhudi zaidi zinahitajika ili kuendelea kuwahamasisha wazazi kuwapeleka shule watoto wenye ulemavu.

Sauti ya 1 – Frances Chiwango, Mkurugenzi wa MERODI

Aidha, Chiwango amesema uamuzi wa serikali kuweka mkazo katika elimu jumuishi umesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza unyanyapaa kati ya wanafunzi wenye ulemavu na wasio na ulemavu, akitolea mfano safari yake ya kwanza kuelekea shuleni.

Sauti ya 2 – Frances Chiwango, Mkurugenzi wa MERODI

Vilevile, ametoa wito kwa viongozi wa serikali za mitaa pamoja na maafisa ustawi wa jamii kushirikiana kwa karibu na wazazi na walezi ili kuhakikisha watoto wenye ulemavu wanapata haki yao ya msingi ya elimu.

Sauti ya 3 – Frances Chiwango, Mkurugenzi wa MERODI

Kwa upande wake, Maximilian Makau, mdau wa elimu na mjumbe wa Bodi ya MERODI, ameitaka jamii kuacha kuwaona watoto wenye ulemavu kama mzigo, akisisitiza kuwa wana uwezo wa kujitegemea na kufanikiwa kama watu wengine endapo watapatiwa fursa sawa.

Sauti ya 1 – Maximilian Makau, Mdau wa Elimu na Mjumbe wa MERODI

Makau pia ameitaka serikali kuwaangalia kwa jicho la pekee wazazi wenye watoto wenye ulemavu, hususan kwa kuwawezesha kupitia mikopo au programu maalumu kama ilivyo kwa makundi mengine maalumu, ili kuwasaidia watoto hao kupata elimu bora.

Sauti ya 2 – Maximilian Makau, Mdau wa Elimu na Mjumbe wa MERODI