Jamii FM

Bilioni 114.5 zaboresha sekta ya elimu mkoani Mtwara

28 July 2024, 00:27 am

Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanal Patrick Sawala akitoa hotuba ya katika maadhimisho ya juma la Elimu yaliyofanyika viwanja vya Mashujaa mjini Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Maadhimisho ya juma la Elimu huambatana na tathmini ya ufaulu ,kutoa mrejesho kwa wadau wa elimu kuhusu mafanikio na changamoto zake Pamoja na kushirikisha wadau wa elimu kuona ,kutambua na kuthamini kazi za walimu na wanafunzi shuleni.

Na Musa Mtepa

Serikali imetoa zaidi ya Bilioni 114.5 katika kipindi cha miaka mitatu kwa ajili ya maendeleo katika  sekta ya Elimu  mkoani Mtwara.

Hayo yamesemwa leo July 27, 2024 na mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Patrick Sawala kwenye kilele cha maadhimisho ya Juma la Elimu liliofanyika katika viwanja vya Mashujaa mjini Mtwara ambapo  amesema kuwa kati ya hizo  shilingi Bilioni 76.6 ni kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya Elimu na kiasi cha Bilioni 37.9 kwa ajili ya kugharamia  Elimu Msingi bila malipo na vinginevyo.

Sauti ya mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Patrick Sawala
Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanal Patrick Sawala akimkabidhi Tuzo mkuu wa utumishi Jeshini Meja Jeneral Marco Gaguti kwa mchango wake katika sekta ya Elimu Mkoani Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Aidha Kanali Sawala amesema mkoa wa Mtwara umeendelea kudumisha utamaduni wa kuadhimisha juma la Elimu na kutoa tuzo mbalimbali ikiwa ni sehemu ya hamasa kwa Shule ,Walimu ,Wanafunzi wanaofanya vizuri Pamoja na kutambua mchango wa wadau wengine wanaochangia uboreshaji wa  sekta ya Elimu katika mkoa wa Mtwara.

Sauti ya 2 Kanali Patrick Sawala mkuu wa mkoa wa Mtwara

Kwa upande wake mkuu wa utumishi Jeshini Meja Jenerali Marco Gaguti mgeni mwalikwa ambaye pia aliwahi kuwa mkuu wa mkoa wa Mtwara katika hotuba yake  amewashukuru wanamtwara kwa mwaliko wa kuhudhuria maadhimisho hayo huku akiwapongeza viongozi kwa maendeleo makubwa wanayofanya katika nyanja mbalimbali .

Sauti ya Meja Jenerali Marco Gaguti mkuu wa utumishi Jeshini
Mkuu wa utumishi Jeshini Meja Jenerali Marco Gaguti akizungumza na Mwanafunzi wa shule ya sekondari Mtwara Ufundi mwenye mahitaji maalumu katika maadhimisho ya juma la Elimu(Picha na Musa Mtepa)

Naye afisa Elimu mkoa wa Mtwara John Lupenza amesema kuwa katika kuboresha hali ya Elimu kumekuwepo na changamoto katika ufuatiliji na usimamizi wa ufundishaji na ufunzaji kwa baadhi ya mamlaka ya serikali za mitaa kutofanyika ipasavyo Pamoja na baadhi ya wazazi  kutoshiriki kikamilifu katika usimamizi na uwezeshaji wa Watoto katika masomo.

Sauti ya John Lupenzi afisa Elimu mkoa wa Mtwara

Maadhimisho ya juma la Elimu 2023/2024 yameenda sambamba na ugawaji wa zawadi ya Baiskel,Vyeti,Fedha,pikipiki na Kompyuta kwa waliofanya vizuri katika kipindi hicho.