Jamii FM

SIDO Mtwara yawataka wajasiriamali kukuza Biashara kidijitali

25 February 2026, 09:42 am

Mkuu wa wilaya ya Mtwara Abdalla Mwaipaya akizungumza wakati ya mafunzo ya uingezaji thamani uliofanyika february 24,2026 mjini Mtwara(Picha na Gregory Milanzi)

Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdallah Mwaipaya, amewahimiza wajasiriamali kuongeza thamani ya bidhaa na kutumia teknolojia, ikiwemo akili mnemba, kukuza biashara zao. Mafunzo hayo yaliandaliwa na SIDO kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuwawezesha kibiashara

Na Gregory Millanzi

Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdallah Mwaipaya, amewataka wajasiriamali kuongeza thamani ya bidhaa zao ili kuongeza kipato, pamoja na kutumia mitandao ya kijamii kujitangaza na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Mwaipaya ameyasema hayo Februari 24, 2026, wakati akifungua semina ya utambuzi wa bidhaa, viwanda na matumizi ya akili mnemba (Artificial Intelligence), iliyofanyika katika Ukumbi wa Benjamini Mkapa, Chuo Kikuu cha MUST Mtwara (zamani Chuo cha Ualimu TTC Kawaida).

Sauti ya Abdallah Mwaipaya – Mkuu wa Wilaya ya Mtwara

Kwa upande wake, Meneja wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) Mkoa wa Mtwara, Merina Mkuchu, amesema lengo la semina hiyo ni kuwatambua wajasiriamali wa Manispaa ya Mtwara na kuwapatia elimu ya kufanya biashara kidijitali badala ya kufanya biashara kwa mazoea.

Mkuchu ameongeza kuwa kwa sasa wanaandaa kanzidata ya kuwatambua wajasiriamali hao ili kuwaunganisha na wadau mbalimbali wanaofika Mtwara kutafuta washirika wa biashara. Pia, SIDO inaandaa kongani la viwanda katika kila wilaya kwa lengo la kuwaunganisha wajasiriamali na kukuza ushirikiano miongoni mwao.

Sauti ya Merina Mkuchu – Meneja SIDO Mkoa wa Mtwara

Naye Afisa Uhusiano kwa Umma kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH), Feisal Abdul, amewahimiza wajasiriamali kuchangamkia fursa zinazotolewa na Serikali kupitia Mfuko wa Uendelezaji Ubunifu (Samia Fund), unaolenga kuwajengea uwezo na kuwapatia ruzuku za kuendeleza bunifu zao.

Sauti ya Feisal Abdul – Afisa Uhusiano COSTECH

Aidha, kampuni ya Scan Code imetoa mafunzo kwa wajasiriamali wa Mtwara kuhusu matumizi ya Scan Code na akili mnemba katika kujitangaza na kupanua masoko ya biashara zao.

Abdulwahid Khamis, mkufunzi kutoka Scan Code, ameeleza faida za teknolojia hiyo na namna inavyoweza kuwasaidia wajasiriamali kuongeza wigo wa soko na mapato.

Sauti ya Abdulwahid Khamis – Mtaalamu wa Mafunzo kutoka Scan Code