Jamii FM
Jamii FM
23 May 2025, 16:51 pm

Hii ilikuwa ni kufunga mafunzo ya kilimo bora cha mazao kwa wakulima vijana waliopo katika kata saba za Manispaa ya Mtwara Mikindani ambapo zaidi ya vijana wa kike na wakiume 700 wamenufaika na mafunzo hayo
Na Musa Mtepa
Zaidi ya wakulima 700 vijana na wanawake kutoka kata saba za Manispaa ya Mtwara Mikindani wamenufaika na mafunzo ya kilimo bora yaliyotolewa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kupitia kituo chake cha Naliendele kwa kushirikiana na Chuo cha Kilimo MATI – Naliendele.
Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, Ndugu Bakari Kidunda, aliyemwakilisha Mkurugenzi wa TARI Naliendele, amesema kuwa lengo la mafunzo hayo ni kuongeza uzalishaji na tija katika sekta ya kilimo kwa manufaa ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla

Aidha Kidunda amesema kuwa mafunzo haya yamefanyika katika kata saba za Manispaa ya Mtwara Mikindani, yakifanikisha lengo la kuwafikia vijana zaidi ya 700.
Kidunda ameongeza kuwa TARI Naliendele ina jukumu la kufanya tafiti za mazao ya kilimo, kutatua changamoto za wakulima, na kuhakikisha teknolojia na matokeo ya tafiti yanawafikia wadau muhimu ambao ni wakulima.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa mtaa wa Pwani C, kata ya Naliendele, Bw. Daudi Katibula ameshukuru kwa mafunzo hayo akisema kuwa yataongeza thamani ya mazao kama mboga mboga na korosho, na hivyo kuinua uchumi wa wakulima wadogo.
Regani Kinanda, mkufunzi kutoka Chuo cha Kilimo MATI Mtwara, ameeleza kuwa jitihada hizi ni sehemu ya utekelezaji wa agenda ya mwaka 2030 ya kuongeza mchango wa sekta ya kilimo kwenye pato la taifa kwa asilimia 10.
Naye Abdala Fadhili, kijana na mkulima kutoka kata ya Naliendele amesema mafunzo hayo ni fursa kwa vijana kuongeza thamani ya mazao na kuboresha uzalishaji wa kilimo cha kisasa.