Jamii FM
Jamii FM
22 July 2025, 16:44 pm

Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) imesema uzalishaji wa korosho umeongezeka hadi tani 528,000 msimu wa 2024/2025, kutokana na pembejeo za ruzuku. Mapato ya kigeni pia yameongezeka.
Na Musa Mtepa
Utoaji wa pembejeo za ruzuku kwa wakulima wa korosho umeleta mapinduzi makubwa katika uzalishaji wa zao hilo nchini Tanzania, ambapo uzalishaji umeongezeka kutoka tani 189,000 msimu wa 2022/2023 hadi kufikia tani 528,000 msimu wa 2024/2025.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake July 21, 2025, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania (CBT), Bw. Francis Alfred, amesema mafanikio haya yanatokana na jitihada za serikali kutoa pembejeo bure kwa wakulima, hatua iliyowapa ari na kuongeza tija shambani.
Bw. Alfred ameongeza kuwa pamoja na mafanikio kwa wakulima, soko la korosho nchini limeendelea kuimarika, hali iliyosaidia kuongeza mapato kupitia fedha za kigeni ambapo katika msimu wa 2023/2024, mauzo ya korosho nje ya nchi yalifikia dola milioni 221.3 za Kimarekani, huku msimu wa 2024/2025 thamani hiyo ikipanda hadi dola milioni 587.7.

Katika hatua nyingine, Serikali kupitia Bodi ya Korosho imeanzisha kongani la viwanda katika Kijiji cha Maranjei kwa lengo la kuongeza thamani ya korosho zinazozalishwa nchini na kuimarisha soko la ndani na nje.
Aidha, uamuzi wa Serikali ya Awamu ya Sita kutaka korosho ghafi zisafirishwe kupitia Bandari ya Mtwara umechochea ukuaji wa uchumi katika mikoa ya Kusini.