Jamii FM

Tells One ,kuinua  Vikundi vya wabangua Korosho Mahuta

16 December 2025, 16:59 pm

Waziri wa kilimo Daniel Chongolo akipata maelezo kutoka kwa moja ya wafanyakazi wa kituo na kiwanda cha kubangua Korosho Mahuta wilayani Tandahimba (Picha na Musa Mtepa)

Ujenzi wa kiwanda cha Tells One General Supply  Mahuta wilayani Tandahimba mkoani Mtwara umeleta faraja kwa akina mama na wabanguaji wadogo wa korosho. Kiwanda hicho kimewezesha upatikanaji wa soko, ajira na kuboresha maisha ya wananchi hususan wanawake wa eneo hilo

Na Musa Mtepa

Vikundi vya akina mama na wabanguaji wadogo wa korosho  Mahuta wilayani Tandahimba mkoani Mtwara vimeeleza kufurahishwa kwao na ujenzi wa kiwanda pamoja na kituo cha kuwasaidia kupata soko na ajira cha Tells One General Supply.

Wakizungumza kuhusu manufaa wanayoyapata kutokana na uwepo wa kiwanda hicho, Bi Amina Mande na Bi Amina Makwangu, ambao ni wafanyakazi wa kiwanda hicho, wamesema kuwa kiwanda kimekuwa msaada mkubwa katika kutatua changamoto zao za kimaisha ikiwemo kusomesha watoto na kujikimu katika mahitaji ya kila siku.

Sauti ya Bi Amina Mande, mfanyakazi wa kiwanda cha Tells One General Supply
Baadhi ya wafanyakazi wa Tells One wakichambua Korosho karanga zilizopokelewa kutoka kwa vikundi vya wabangauaji wadogo Mahuta (Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, msimamizi wa kiwanda hicho, Bi Mariamu Chilongo, amesema dhamira ya kuanzishwa kwa kiwanda hicho ni kuwasaidia wabanguaji wadogo wa korosho, hususan akina mama, ambao hapo awali walikuwa wakikumbana na changamoto ya upatikanaji wa masoko. Amesema kiwanda hicho hupokea korosho zilizobanguliwa, kuziboresha na kuzisafirisha kwenda sokoni.

Sauti ya Bi Mariamu Chilongo, Msimamizi wa Kiwanda
Mariamu Chilongo Msimamizi wa kituo na kiwanda cha kuwasaidia wabanguaji wadogo Mahuta wilayani Tandahimba (Picha na Musa Mtepa)

Aidha, Bi Mariamu amesema kuwa pamoja na kupokea korosho kutoka katika vikundi mbalimbali, kiwanda hicho tayari kimeajiri wafanyakazi wa kike wasiopungua 50, huku matarajio yakiwa ni kuongeza idadi hiyo hadi kufikia wafanyakazi 500 siku za usoni.

Sauti ya Bi Mariamu Chilongo, Msimamizi wa Kiwanda

Kituo na kiwanda cha Tells One General Supply (TOGS) kimejengwa katika kijiji cha Mahuta wilayani Tandahimba mkoani Mtwara, kikiwa na lengo la kusaidia upatikanaji wa soko la korosho kwa vikundi vidogo vya ubanguaji pamoja na kutoa ajira kwa akina mama wa eneo hilo.