Jamii FM

Wananchi waililia serikali urejeshwaji wa Mv Kilambo

14 July 2025, 22:16 pm

Abiria wakipanda kwenye Boti tayari kuelekea upande wa nchi ya Msumbiji (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Kilambo, Mtwara, wameiomba serikali kurejesha feri ya MV Kilambo ili kuondoa adha ya usafiri, gharama kubwa na hatari ya kutumia viboti vidogo kuvuka mpaka kuelekea Msumbiji

Na Musa Mtepa

Baadhi ya wananchi na watumiaji wa kivuko cha Kilambo kuelekea nchi jirani ya Msumbiji wameiomba serikali kuchukua hatua za haraka kurejesha feri ya MV Kilambo ili kuondoa usumbufu na gharama kubwa wanazokumbana nazo kwa sasa.

Wakizungumza na Jamii FM Radio, wakazi hao wamesema hali ya usafiri katika eneo hilo si ya kuridhisha, kwani hulazimika kutumia viboti vidogo kuvuka mpaka huo wa maji, ambavyo si salama na vinagharimu fedha nyingi ukilinganisha na huduma ya awali ya feri.

Ahamadi Hassani na Ahamadi Fuka, wakazi wa Kijiji cha Kilambo katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini, wanasema kuwa kutokuwepo kwa feri hiyo kunawalazimu kutumia vijiboti vidogo ambavyo vinaweka maisha yao hatarini na kuongeza gharama ya usafiri.

Sauti ya Ahamdi Hassani na Ahamadi Fuka wakazi wa Kijiji cha Kilambo

Kwa upande wake, Rajabu Athumani Salumu, bodaboda kutoka kijiji hicho, ameeleza kuwa ukosefu wa chombo cha uhakika cha kusafiria umepelekea mlundikano wa mizigo na abiria, huku wengine wakilazimika kulala eneo hilo kwa zaidi ya siku tatu wakisubiri usafiri.

Sauti ya Rajabu Athumani Salumu bodaboda wa kijiji kilambo
Abiria wakiwa kwenye Boti kuelekea nchini Msumbini (Picha na Musa Mtepa)

Fatuma Bakari, mkazi wa kijiji cha Singa kilichopo nchini Msumbiji, anasema kuwa ucheleweshaji mkubwa unaosababishwa na kutokuwepo kwa kivuko umekuwa changamoto kwa wakazi wa pande zote mbili za mpaka.

Sauti ya Fatuma Bakari mkazi wa Kijiji cha Singa Msumbiji.
Baadhi ya bidhaa zilizonunuliwa katika Soko la Mtwara tayari kusafirishwa kuelekea vijiji vilivyopo wilaya ya Palma nchini Msumbiji (Picha na Musa Mtepa)

Mfaume Faila, mfanyakazi wa kampuni ya uchimbaji mafuta huko Palma, Msumbiji, ameongeza kuwa gharama ya kuvuka imepanda sana, na hali hiyo inawaathiri wafanyabiashara na abiria wa kawaida.

Sauti ya Mfaume Faila mkazi Palma nchini Msumbiji
Viroba vya unga vikisubiri boti visafirishwe kwenda wilayani Palma Nchini Msumbiji(Picha na Musa Mtepa)