Jamii FM

Zitto aahidi Mtwara kuwa kitovu cha uchumi wa SADC

13 July 2025, 15:42 pm

Kiongozi wa ACT Wazalendo Zito Kabwe akiwa katika mkutano na Wananchi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani kwenye viwanja vya Sinani (Picha na Musa Mtepa)

Zitto Kabwe wa ACT Wazalendo amewahamasisha wananchi wa Mtwara kushiriki uchaguzi mkuu Oktoba 2025, akisisitiza umuhimu wa kuchagua viongozi wa chama hicho ili kuleta maendeleo.

Na Musa Mtepa

Kiongozi wa chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe, amewaasa wananchi wa Mtwara kushiriki kwa wingi na kikamilifu katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba 2025, akisisitiza kuwa ni haki yao ya kisheria.

Akizungumza Julai 12, 2025 katika viwanja vya Sinani Manispaa ya Mtwara Mikindani, katika oparesheni ya chama hicho iitwayo Maji Maji, Zitto amesema kuwa mikoa ya Lindi na Mtwara imebarikiwa kuwa na rasilimali nyingi ikiwemo gesi asilia na zao la korosho, lakini wananchi wa maeneo hayo bado wanaishi maisha magumu ambayo hayaendani na utajiri wa mikoa hiyo.

Sauti ya 1 Zito Kabwe kiongozi wa ACT Wazalendo

Aidha, Zitto ameongeza kuwa endapo wananchi wa Mtwara wataamua kuwapa ridhaa viongozi wa chama chake, watahakikisha mkoa huo unageuka kuwa kitovu cha maendeleo ya kiuchumi kwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), kwa kutumia bandari ya Mtwara na mpaka wa Msumbiji kikamilifu kwa maendeleo ya wananchi.

Sauti ya 2 Zito Kabwe kiongozi wa ACT Wazalendo

Naye Waziri Kivuli wa Uchukuzi wa ACT Wazalendo, Halima Nabalang’anya, amesema kuwa chama hicho kipo tayari kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu na kuwaomba wananchi wa Mtwara kufanya maamuzi sahihi ya kuwachagua wawakilishi wa ACT Wazalendo.

Sauti ya 1 Halima Nabalang’anya Waziri kivuli wa uchukuzi
Halima Nabalang’anya waziri kivuli wa uchukuzi ACT Wazalendo akizungumza na wananchi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani (Picha na Musa Mtepa)

Amesema moja ya changamoto kubwa ni miundombinu ya mkoa wa Mtwara kutokulingana na kiwango cha uchumi uliopo, jambo ambalo ACT Wazalendo inalenga kulitatua iwapo itapewa dhamana ya kuongoza.

Sauti ya 2 Halima Nabalang’anya Waziri kivuli wa uchukuzi
Baadhi ya Wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa ACT Wazalendo July 12,2025 katika viwanja vya Sinani Manispaa ya Mtwara Mikindani (Picha na Musa Mtepa)