Jamii FM
Jamii FM
12 March 2025, 08:55 am

Zahanati ya Makome B inayopatikana kata ya Mbawala halmashauri ya wilaya Mtwara ilizinduliwa na kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa Ndugu Mzee Mkongea Ali Tarehe 06.10.2019 ikiwa na majengo mawili ambayo ni jengo la zahanati na nyumba moja ambayo wanaishi watumishi wa zahanati hiyo.
Na Musa Mtepa
Mwaka 2023, Jamii FM kwa kushirikiana na ESRF (Economic and Social Research Foundation) walifanya utafiti kuhusu hali ya upatikanaji wa huduma za afya na changamoto zake katika baadhi ya zahanati za Halmashauri ya Mtwara Mjini na Vijijini.
Utafiti huo ulionesha changamoto kadhaa ikiwemo uhaba wa wahudumu wa afya, nyumba za kuishi watumishi wa afya, uhaba wa maji, na kutokuwepo kwa umeme wa uhakika.
Katika utafiti huo, zahanati ya Makome B ilikuwa miongoni mwa zahanati zilizofanyiwa utafiti, ambapo ilibainika kuwa zahanati hiyo ilikuwa na changamoto kubwa za uhaba wa maji, nyumba moja kwa watumishi wawili, na kutokuwepo kwa umeme wa uhakika.
Katika jitihada za kufuatilia utekelezaji wa ahadi zilizotolewa na serikali, Jamii FM kwa kushirikiana na ESRF walirudi tena katika zahanati ya Makome B mnamo Januari 30, 2025, kujionea hali halisi ya utekelezaji wa ahadi hizo.
Agneter Adespery, Mganga Mfawidhi wa zahanati ya Makome B, ameeleza kuwa changamoto za awali bado zipo, ingawa kwa upande wa umeme wa uhakika walifanikiwa kuuweka kwenye zahanati hiyo.
Agneter Adespery ameongeza kuwa, kutokana na uhaba wa maji na nyumba moja inayotumiwa na watumishi wawili, ameiomba serikali na wadau wa maendeleo kuangalia namna ya kutoa msaada katika kuhakikisha watumishi wanaishi katika nyumba zao binafsi
Wananchi wa kijiji cha Makome B wamekiri kuwepo kwa changamoto hiyo ya wahudumu wa afya kuishi katika nyumba moja na wameeleza shukrani zao kwa serikali kwa juhudi za kuunganisha umeme wa uhakika katika zahanati hiyo.
Hata hivyo, wametoa wito kwa serikali kuangalia changamoto zingine zilizobaki.
Bakari Mkanjalanga Mwenyekiti wa Kijiji cha Makome B anasema kuwa kitendo cha watumishi kuishi nyumba moja ni kikwazo kikubwa ambacho yeye kama kiongozi alilifikisha halmashauri ya Mtwara Vijijini na hadi kufikia hii leo bado hawajatatuliwa changamoto hiyo.
Kwa upande mwingine, Dkt. Joel Lazaro, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara, amezungumzia hatua zilizochukuliwa na serikali katika kukabiliana na changamoto hizo.
