Jamii FM

Mtoto  Yasri (14) ahofiwa kupoteza maisha mto mambi Mtwara

10/03/2026, 10:02

Mwonekano wa Mto Mambi unaomwaga maji Bahari ya Lindi (Likonde Namahyavi kijiji cha Ndumbwe) ukiwa umefurika maji( Picha na Musa Mtepa)

Mtoto Yasri Hamisi (14) wa kijiji cha Ndumbwe, Mtwara, anahofiwa kufariki baada ya kutumbukia mtoni alipoteleza akijaribu kugusa maji wakati akiwa na wenzake. Wananchi na vikosi vya uokoaji wanaendelea na juhudi za kumtafuta

Na Musa Mtepa

Mtoto Yasri Hamisi, mwenye umri wa miaka 14, mkazi wa kijiji cha Ndumbwe, wilaya na mkoa wa Mtwara, anahofiwa kupoteza maisha baada ya kutumbukia katika mto unaopita kijijini hapo ukitokea Bwawa la Kitere kuelekea Bahari ya Hindi upande wa Ndumbwe.

Inaelezwa kuwa Yasri aliambatana na wenzake watatu mnamo March 7, 2026 kwenda katika mto huo kwa ajili ya kufanya shughuli za uvuvi. Hata hivyo, walipofika mtoni walibadili maamuzi ya kuvua samaki na kuamua kuoga. Mmoja wao aliwaonya wenzake kuwa maji yalikuwa mengi na yana kasi hivyo yeye hangeweza kuoga.

Inadaiwa kuwa Yasri alipokuwa akijaribu kugusa maji kwa mguu ndipo alipoteleza na kutumbukia mtoni na kuzama.

Wakizungumzia tukio hilo jana, March 9, 2026, wakazi wa kijiji cha Ndumbwe wamesema wanaendelea na juhudi za kumtafuta kijana huyo kwa kufuata mwelekeo wa maji yanakoelekea kuchanganyika na maji ya Bahari ya Hindi.

Sauti ya wananchi wa kijiji cha Ndumbwe
Wananchi wa kijiji cha Ndumbwe wakiendelea na utafutaji wa Mtoto Yasri Hamisi katika eneo la Mikoko mwelekeo wa maji yanatoka Mto Mambi(Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, mwenyekiti wa kijiji cha Ndumbwe Ali Mshamu amekiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa baada ya kupata taarifa alitoa taarifa kwa wananchi wa kijiji kizima ili kuanza jitihada za kumtafuta kijana huyo. Hata hivyo hadi kufikia jana, March 9, 2026, bado hawajafanikiwa kumpata.

Sauti ya Ali Mshamu mwenyekiti wa kijiji

Akizungumzia tukio hilo, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Ambrosi Ndunguru amesema kuwa baada ya kupokea taarifa ya tukio hilo, timu ya uokoaji ya jeshi hilo ilifika katika kijiji cha Ndumbwe na kuanza operesheni ya kumtafuta kijana huyo, lakini hadi sasa hawajafanikiwa kumpata baada ya juhudi za siku mbili huku akisema kuwa zoezi la utafutaji litaendelea kwa siku ya tatu.

Aidha, Mrakibu Ndunguru ametoa wito kwa wakazi wa eneo hilo kuepuka kusogelea mto huo kwa shughuli za uvuvi au kilimo kwa sasa, kutokana na kufurika kwa maji yenye kasi yanayotoka katika Bwawa la Kitere pamoja na vijiji vya pembezoni.

Sauti yaAmbrosi Ndunguru mrakibu msaidizi wa zimamoto